WANAWAKE
zaidi ya 300 wamejitokeza kupewa semina ya uzazi wa mpango, saratani ya
shingo ya kizazi na elimu kuhusu ugonjwa wa Ukimwi iliyoandaliwa na
Shirika linalotoa Elimu ya Afya la PSI Tanzania mjini Dodoma.
Mbali ya
kushiriki katika semina hiyo, wanawake 90 walipima afya zao papo hapo
baada ya kupata elimu, huku waandaaji wakisema uelewa mdogo ni kiini
kikubwa cha wanawake kushindwa kupima afya zao ili kujitambua.
Akizungumza
na waandishi wa habari wakati wa semina hiyo, Meneja wa Huduma ya Uzazi
wa Mpango wa PSI, Catherine Paul alisema bado uelewa kuhusu uzazi,
saratani ya shingo ya kizazi, Ukimwi, malezi ya watoto ni tatizo kwa
wanawake wa mijini na vijijini.
“Kwa
kweli mwitikio umekuwa mkubwa kuliko hata vile tulivyotarajia.Kama
inavyofahamika ugonjwa wa saratani ya shingo ya kizazi hivi sasa ni
tishio kubwa na takwimu zinaeleza kuwa Tanzania inaongoza kwa kuwa na
wagonjwa wengi kuliko nchi nyingine za Afrika Mashariki,” alisema.
“Leo
tunashuhudia na kufurahi kuona kuwa wanawake hawa zaidi ya 300
wamekutana hapa ili kubadilishana mawazo na kupata elimu kwa mambo
yanayowahusu hatua itakayosaidia kwa kiasi kikubwa kubadili mifumo yao
ya maisha baada ya kujitambua,” alisema.
Kwa
upande mwingine, Mratibu wa Mradi wa Afya ya Mama na Mtoto, Khadija
Ameir alisema PSI imekuwa inatoa elimu kuhusu masuala hayo katiika
maeneo mbalimbali ya mijini na vijijini kwa lengo la kumkomboa mwanamke
na kustawisha maisha yake.
Alisema
katika maeneo ya vijijini Shirika hilo limekuwa likiendesha kampeni ya
nyumba kwa nyumba ili kuwafiki wanawake na kuwapa elimu kuhusu uzazi wa
mpango, saratani ya shingo ya kizazi, Ukimwi na malezi ya Mama na
Mtoto, hatua ambayo imeongeza idadi ya wanawake ambao sasa wanatambua
kuhusu afya ya uzazi.
“Ikumbuke
kwamba PSI inawatumia wataalamu katika kufikisha elimu hii kwa wanawake
hatua ambayo imesaidia kupunguza idadi ya vifo vya wanawake kutokana na
masuala ya uzazi, Ukimwi na hata saratani ya shingo ya kizazi, huku pia
vifo vya watoto chini ya miaka mitano vikipungua,” alisema Ameir.
Akizungumza,
Mratibu wa mafunzo hayo kutoka Asasi ya Women in Balance (Mizania ya
Wanawake), Vida Mndolwa alisema mwitikio wa wanawake katika kujitokeza
kupata elimu wa afya ya uzazi, Ukimwi na saratani ya shingo ya kizazi
umekuwa mkubwa kila mahala ambapo wanafika kutoa elimu hiyo.
“Kama
mnavyoona hapa Dodoma mwitikio umekuwa ni mkubwa sana na tunashukuru
kuona wanawake wamejitokeza ili kupata fursa ya kukutana na wataalamu wa
huduma za afya suala ambalo litaongeza uwezekano wa wao kujitambua na
kuwa na maisha yaliyo bora na salama,” alisema Mndolwa.
Mmoja wa
washiriki Mwanajuma Othman Mtuli alisema;” Ni zaidi ya elimu, ni zaidi
ya burudani, ni zaidi ya mafunzo. Kwa kweli semina hii imetusaidia
kufahamu kuhusu kujua umuhimu wa malezi ya watoto, kutunza ndoa na hata
ujasiriamali na hivyo tunaishukuru sana PSI kwa mafunzo haya.”