SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Friday, July 11, 2014

Sumaye: Miradi mingi mibovu ni pasenti za wakubwa

sumaye_6a536.jpg
Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye jana aliamua kutoa ya moyoni wakati alipobainisha kuwa kujengwa kwa kiwango cha chini kwa miradi mingi, kunatokana na wakubwa kupewa 'pasenti' za rushwa na kampuni zinazoshinda zabuni hizo.
Sumaye, ambaye amekuwa kimya kwa muda mrefu, alisema hayo jana katika Chuo cha Benki Kuu jijini Mwanza wakati akizindua kikundi cha vijana kinachoitwa Tanzania Youth Development Centre (TYDC), tawi la Mwanza.

"Hii ni rushwa ya ulafi. Hii wananchi wanaweza wasiione moja kwa moja, lakini ina maumivu makali na mabaya ya muda mrefu kwa nchi," alisema mtendaji huyo mkuu wa zamani wa serikali.
"Hii ni rushwa ya wakubwa wanaotoa uamuzi kwa miradi mikubwa ya taifa na muhusika anawekewa asilimia zake fulani za gharama za mradi kama fedha zake binafsi na fedha hizi au chochote walichokubaliana wakapeana kwa utaratibu wowote watakaokubaliana," aliongeza Sumaye.(P.T)
"Hapa lazima mradi husika utajengwa chini ya kiwango kwa sababu kubwa mbili; kwanza, sehemu ya fedha za mradi zimeingia mfukoni mwa mtu kwa hiyo ili zilizobaki, ni lazima zitakuwa za kurashiarashia mradi; pili; ambaye angesimamia mradi huo anafumbwa macho, haoni tena, amezibwa masikio hasikii tena na amefungwa mdomo hasemi tena.
"Rushwa hii ina gharama kubwa kwa uchumi kwa sababu miradi tunayokopea fedha nyingi au hata kama ni fedha zetu, inashindwa kukamilika kwa wakati au inakamilishwa tu, lakini haina maisha marefu kama ambavyo ilitegemewa."
Sumaye ambaye hakuweka bayana miradi hiyo, alisema:
"Hasara nyingi ni kuwa zile kampuni zenye uwezo wa kufanya kazi bila rushwa haziwezi kupata kazi kwa sababu ya kuzidiwa ujanja na watoa rushwa. Hili nalo ni la hatari sana kwa uchumi wetu."
Dawa za kulevya
Akizungumzia dawa za kulevya, Sumaye, ambaye ni waziri mkuu mstaafu pekee aliyeshika wadhifa huo kuanzia mwaka 1995 hadi 2005, alisema biashara ya dawa za kulevya hufanywa na watu wazito ama kwa fedha zao au kwa madaraka yao.
Alisema kwa sasa Tanzania inaonekana kuwa kituo muhimu cha kupitishia dawa hizi kwenda na kutoka nchi nyingine.
"Hii siyo sifa nzuri kwa nchi yetu... ukiachilia mbali madhara ya kupitishia nchini mwetu, dawa hizi huathiri vijana na kuwageuza mazezeta kwa baadhi ya wanaotumia."
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

Post a Comment