SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Sunday, October 13, 2013

UONGOZI WA SHIRIKA LA CHANGAMOTO ZA MILENIA –MILLENIUM CHALLENGE CORPORATION (MCC) WAKUTANA NA UJUMBE KUTOKA TANZANIA

Ujumbe wa Tanzania na Viongozi wa MCC katika majadiliano.
Viongozi wa Tanzania ukisikiliza kwa makini uongozi wa MCC hawapo pichani wakati wa majadiliano. Kutoka kushoto ni Katibu Mkuu Wizara ya Fedha Jamhuri ya Muungano Dkt. Servacius Likwelile, Balozi wa Tanzania Marekani na Mexico Mhe. Liberata Mulamula, Waziri wa Fedha wa Jamhuri ya Muungano Mhe. Dkt. Wiliam Mgimwa, Waziri wa Fedha Zanzibar Mhe. Yusuph Mzee,  Katibu Mkuu Wizara ya Fedha Zanzibar Bw. Khamis Mussa.
Ujumbe wa Tanzania wakifuatilia majadiliano na MCC mjini Washington, kutoka kulia ni  Kamishna wa Fedha za Nje Jamhuri ya Muungano Bw. Said Magonya, Kamishna wa Fedha za Nje Zanzibar, Bi. Bihindi Nassor, Naibu Ganana wa BOT Dkt. Natu Mwamba pamoja na Mkurugenzi wa Mipango Zanzibar.

Picha zote na Bi. Ingiahedi Mduma na Bi Eva Valerian 
Washington DC
 ****

UONGOZI WA SHIRIKA LA CHANGAMOTO ZA MILENIA –MILLENIUM CHALLENGE CORPORATION (MCC) WAKUTANA NA UJUMBE KUTOKA TANZANIA

Wakati Mikutano ya mwaka ya Shirika la fedha la kimataifa na makundi ya benki ya Dunia ikiendelea hapa mjini Washington DC, Ujumbe kutoka Tanzania watumia nafasi hiyo kukutana na Uongozi wa Millenium Challenge Corporation (MCC) kwa madhumuni ya kujadili mafanikio yaliyopatikana kutokana na  shirika hili la Marekani. MCC awamu ya kwanza ilisaidia sana miradi mbalimabli Tanzania, ambapo walitoa dola milioni 698 ambayo ilielekezwa katika miradi ya barabara, umeme, maji pamoja na miradi ya barabara Zanzibar pamoja na uwanja wa ndege wa Mafia (Mafia Airport).

Akizungumza na vyombo vya Habari mjini hapa,  Waziri wa Fedha Dkt. Wiliam Mgimwa alisema kuwa “Miradi hiyo yote ya MCC ya kwanza ilikwenda vizuri sana na tunamaliza nao mkataba tukiwa tumefanikiwa sana katika ujenzi wa miradi hiyo”. 

Aidha Mgimwa aliendelea kutoa ufafanuzi akisema kuwa “lengo kubwa la kukutana na Uongozi wa MCC ni kuangalia mafanikio yaliyopatikana katika miradi waliyoianzisha na ni nini tumejifunza kutoka  katika hiyo miradi  ili tuepuke matatizo katika miradi mingine inayofuata”.

Katika majadiliano hayo ujumbe wa Tanzania ulipata fursa ya kuzungumzia miradi ya  MCC ya  awamu ya pili ambapo MCC wamekubali kuisaidia Tanzania kueneza umeme vijijini hasa vijiji vikubwa vinavyozalisha mazao kwa wingi  na vijiji vyenye watu wengi pamoja na  kujenga barabara katika maeneo ya uzalishaji.

“Hii itakuwa nafasi ya Tanzania kuweza kusaidia kueneza umeme vijijini ambapo wananchi wetu watapata nafasi ya kutumia umeme huo katika miradi midogo midogo na vile vile kwa ajili ya kuhakikisha kuwa miradi ya barabara hasa katika vijiji vinavyozalisha mazao wanaweza kupokea pembejeo na baada ya kuvuna kuweza kufikisha mazao yao kwa walaji.” Alifafanua  Mgimwa.   

Hali ya hewa ya mjini hapa ni baridi kiasi na manyunyu ya hapa na pale.

Imetolewa na:
Ingiahedi Mduma
Msemaji Mkuu
Wizara ya Fedha
Washington D.C
13/10/2013

0 comments:

Post a Comment