SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Monday, March 7, 2011

Askofu Aipasha Serikali ya Rais Kikwete

Askofu Charles Mjema wa KKKT ya Dayosisi ya Pare akifuatilia hoja za mkutano mkuu wa 14 wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Karanga mjini Moshi
Na Daniel Mjema,Moshi
ASKOFU wa Dayosisi ya Pare ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Charles Mjema amesema ubabaishaji katika uendeshaji wa nchi unaofanywa na baadhi ya watendaji wakuu serikalini, ndio unaoitafuna nchi kwa sasa. Wakati Askofu Mjema akitoa kauli hiyo, Mchungaji kiongozi wa Usharika wa Karanga wa KKKT mjini Moshi, Fred Njama amesema mkakati wa Serikali ya Rais Jakaya Kikwete wa kufikia maisha bora kwa kila Mtanzania unatia mashaka kuliko matumaini.
Viongozi hao waandamizi wa KKKT walitoa kauli hizo mjini Moshi mwishoni mwa wiki iliyopita, katika mkutano mkuu wa 14 wa Usharika wa Karanga uliopo Soweto ambapo mgeni rasmi alikuwa Askofu Mjema.
Kauli za viongozi hao zimekuja kipindi ambacho kuna mjadala mkali nchini kuhusu hali ngumu ya maisha inayotokana na kupanda kwa gharama za mafuta, mgawo wa umeme na ngozeko la bei za bidhaa na huduma mbalimbali.
Miongoni mwa bidhaa zinazolalamikiwa kupanda bei kwa haraka ni sukari ambapo kilo moja inauzwa kati ya Sh2000/ - na 2200/- tofauti na bei ya awali ambapo bidhaa hiyo ilikuwa ikuzwa kati ya Sh1600/- na 1700/- kwa kilo moja.
Kadhalika suala la mgawo wa umeme ni tatizo kubwa hivi sasa kiasi cha kukwaza shughuli za uzalishaji na utoaji wa huduma huku Serikali ikitoa taarifa kwamba mgawo huo unaweza kumalizika rasmi mwezi Julai mwaka huu. 
Jana Askofu Mjema alisema: “Yapo masuala mengi ya ubabaishaji Dowans na mikataba mibovu isiyo na maslahi na nchi… yapo mambo yanayokera mpaka tunajiuliza tunakwenda wapi….kila siku hali inazidi kuwa mbaya kuliko jana yake”.
Askofu huyo alitaja baadhi ya mambo yanayokera Watanzania kuwa ni pamoja na malipo ya Sh94 bilioni kwa kampuni ya kufua umeme wa dharura ya Dowans, michakato ya kuuza ardhi ya wanyonge na kumilikisha migodi kwa wageni.
Bila kumtaja kiongozi yeyote aliyekuwa akimlenga katika hotuba yake hiyo, Askofu Mjema alieleza kushangazwa na kauli ya kiongozi mmoja wa serikali kwamba hamfahamu mmiliki wa Dowans wakati kampuni hiyo ina mikataba na serikali.
“Inakuwaje una mkataba naye mmefanyaje kazi naye halafu unasema humjui?…maana yake ni kwamba watendaji wake aliowaweka hawako makini…hivi kweli mtasema mna Makatibu Wakuu kweli?”alihoji Askofu Mjema.
Maisha ya Wanyonge
Askofu huyo alisema Kanisa limepewa mamlaka na Mungu kutetea wanyonge wa Tanzania wanaokandamizwa na kudhulumiwa na watafanya hivyo hata kama kwa kufanya hivyo itawagharimu maisha.
“Tumepewa mamlaka ya kusema ni lazima tuseme maana Mamlaka tuliyo nayo ni kutoka juu…hatuwezi kufumbia uonevu uendelee halafu tukasema sisi ni kanisa…wajibu wa Kanisa ni Sauti ya Wanyonge,”alisisitiza Askofu Mjema.
Kwa upande wake, Mchungaji Kiongozi Fred Njama alisema kabla ya uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka jana, Wakristo walimuomba Mungu awape viongozi watakaokuwa watumishi wa Taifa la Tanzania na sio mabwana.
“Tuliomba tupate viongozi wenye macho ya rohoni yenye kuona maumivu ya watu wa Mungu…hata hivyo kwa miezi hii michache mkakati wa viongozi wa serikali kufikia matarajio ya wengi unatia mashaka kuliko matumaini,”alisema Njama.
Mchungaji Njama alisema badala yake maisha hivi sasa hayashikiki huku bei za bidhaa zikipanda mara dufu na masuala nyeti kama ya Dowans na mzaha wa majibu ya viongozi wa serikali vinatia shaka umakini wa Serikali.
“Inatia uchungu na kukatisha tamaa…kutokuwa makini kwa utendaji wa serikali na matukio ya kizembe kama yale ya kujirudia kwa milipuko ya mabomu ya Mbagala na baadae Gongolamboto yameleta maafa,”alisema.
Mchungaji Njama aliwaambia wajumbe wa mkutano huo wapatao 150 kuwa mateso kwa Yatima na Wajane na vijana kukosa ajira huku wawekezaji wa Nje wakifaidika na maliasili na Madini ya Watanzania ni mambo yanayokera.
Mkutano huo ulihudhuriwa pia na Wachungaji wa Sharika mbalimbali za KKKT ambapo ilielezwa kuwa mapato ya usharika huo kwa mwaka 2010 yakiwa ni Sh168.2 Milioni kulinganisha na lengo la kupata sh147.4 Milioni. 

0 comments:

Post a Comment