Watu 50 wauawa ajali ya treni Congo

Congo Brazzaville
Congo Brazzaville
Takriban watu 50 wameuawa katika ajali ya treni kusini mwa Congo-Brazzaville.
Mkuu wa mamlaka ya safari za reli nchini humo amesema ajali hiyo ilitokea Jumatatu kilomita 60 kutoka mji wa Pointe-Noire.
Treni hiyo inaamika kupoteza mwelekeo wakati ilipofika karibu na Bilinga na baadhi ya mabehewa yake yakaanguka.
Watu waliokufa wamepelekwa katika vyumba vya kuhifadhi maiti huku waliojeruhiwa wakipelekwa hospitalini.
''Ilitokea ajali mbaya sana ya treni usiku'', Mkuu wa mamlaka ya safari za treni Sauveur Joseph El Bez ameliambia shirika la habari la AFP.''watu wengi wamejeruhiwa na wengine kufa.''
Mshauri wa wizara ya uchukuzi Alphonse Pepa amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo. 
Usimamizi mbaya
Mwandishi wa BBC anasema reli hiyo yenye urefu wa kilomita 500 ilijengwa kati ya mwaka 1920 na 1930 wakati wa enzi ya ukoloni ambapo Ufaransa ilikuwa ikitawala nchi hiyo.
Tangu wakati huo reli hiyo haijakuwa ikisimamiwa vizuri.
Reli kati ya mji mkuu Brazzaville na Pointe-Noire ilifungwa miaka ya tisini wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini humo na tangu ilipofunguliwa kumetokea ajali mbili mbaya.
Ajali hii ndiyo mbaya zaidi kutokea katika siku za hivi karibuni.
Mwishoni mwa juma ndege iliyokuwa imebeba wakurugenzi wa kampuni ya uchimbaji madini kutoka Australia ilianguka na kusababisha vifo vya abiria wote 11.