SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Wednesday, June 23, 2010

Jambazi sugu wa mihadarati akamatwa Jamaica "Dudus"


Christopher Dudus jambazi sugu wa mihadarati Jamaica
Polisi nchini Jamaica wamemkamata kiongozi sugu wa biashara za mihadarati nchini humo Christopher Dudus Coke viungani mwa mji mkuu, Kingston.
Bwana Coke ambaye amekuwa akisakwa kwa muda mrefu, anatakiwa nchini Marekani kwa mashtaka ya ulanguzi wa dawa za kulevya pamoja na biashara haramu za silaha.
Juhudi za kumkamata Coke mwezi jana zilisabisha vurugu nchini humo ambapo watu zaidi ya sabini waliuawa.
Mkuu wa polisi nchini Jamaica, Owen Ellington, alisema kuwa maafisa wake wa polisi wameonywa dhidi ya kutokea vurugu zingine kufuatia kukamatwa kwa bwana Coke.
Huenda akafikishwa mahakamani katika muda wa masaa arobaini na nane.
Bwana Coke alitajwa kama mmoja wa majambazi sugu zaidi duniani, ingawa wafuasi wake wanasema yeye ni kiongozi wa jamii.
**********
Wabunge Nigeria waumizwa bungeni
Solomon Ahwinahwi, mbunge wa Nigeria
Mbunge mmoja Nigeria amevunjika mkono katika fujo zilizotokea bungeni.
Solomon Ahwinahwi ni mmoja wa wawakilishi wanaojaribu kumlazimisha spika aachie madaraka.
Amejeruhiwa wakati vurugu zilipoanza baada ya wafuasi wa spika walipojaribu kutoa mapendekezo ya muswada kuwasimamisha kwenye bunge la wawakilishi.
Mwakilishi mwengine, Doris Uboh, naye alijeruhiwa. Bw Ahwinahwi ametibiwa katika kliniki moja ya bunge hilo kabla ya kupelekwa hospitali.
Mwandishi wa BBC Mohammed Aba mjini Abuja amesema polisi wamejaribu kuwakamata wapiga picha wawili waliopiga picha za fujo lakini baadae waliachiwa huru.
Anasema kundi linalojaribu kumwondoa spika Oladimeji Bankole linajulikana kama Progressives. Wametoka chama tawala cha People's Democrat.
Siasa za Nigeria ziko katika hali tete tangu baada ya kifo cha Rais Umaru Yar'Adua mwezi Mei.
Mpaka sasa haijajulikana iwapo mrithi wake Goodluck Jonathan atawania urais kwenye uchaguzi unaotarajiwa kufanyika mapema 2011.

0 comments:

Post a Comment