SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Friday, September 18, 2015

TATIZO LA UHABA WA MAJI WILAYANI MKURANGA KUWA HISTORIA.

 Mwakilishi wa Kampuni ya Uchimbaji wa Visima ya ZENTAS kutoka Uturuki nchini Tanzania Dkt, Mohammed Akbar Akitoa taarifa za kukamilika kwa kazi ya uchimbaji wa kisima chenye urefu wa mita 541 eneo la Mkwalia, Mkuranga, Pwani leo.Kisima hicho kinauwezo wa kuzalisha maji lita milioni 1.8 kwa siku.
 Maji kutoka katika kisima hicho yakitiririka kufuatia kufanyika kwa majaribio ya kuyatoa maji kutoka ardhini.
 Kiongozi wa waendesha mitambo ya uchimbaji visima wa kampuni ya ZENTAS Bw. Sima Teodor ( kushoto) akitoa maelezo kwa wandishi wa habari kuhusu kazi ya uchimbaji wa kisima hicho katika eneo la mradi wilayani Mkuranga.
 Mtaalam wa mitambo wa Kampuni ya ZENTAS Sahtn Topal ( katikati) akifafanua teknolojia na vifaa vilivyotumika kuchimba kisima hicho.Picha na Aron Msigwa/ MAELEZO.

Na.Aron Msigwa- MAELEZO
Wananchi wa wilaya ya Mkuranga,mkoa wa Pwani wanatarajia kunufaika na mradi mkubwa wa usambazaji wa maji kufuatia kukamilika kwa zoezi la uchimbaji wa kisima cha maji chenye urefu wa mita 541 ambacho kina uwezo wa kuzalisha lita milioni  1.8  kwa siku.

Akitoa taarifa za kukamilika kwa kazi ya uchimbaji wa kisima hicho  mwakilishi wa kampuni ya kuchimba visima ya ZENTAS  kutoka Uturuki nchini Tanzania Dkt.Mohammed Akbar amesema wao kama wataalam wanaendelea na majaribio ya kuyatoa maji kutoka ardhini  jambo ambalo limeonyesha mafanikio makubwa.

 Amesema mtambo wa kuchimba kisima hicho uliwasili eneo la mradi Julai 9 mwaka huu na kuongeza kuwa mara baada ya kuwasili katika eneo la mradi kazi ya uchimbaji ilianza na kubainisha kuwa  sasa kisima hicho kinazalisha kiasi cha lita  76,000 kwa saa na lita milioni  1.8 kwa siku.

Dkt. Akbar amesema endapo maji hayo yataunganishwa kwenye miundombinu ya maji ya mji huo yatakidhi mahitaji ya maji ya mji wa Mkuranga ambayo ni lita laki  Sita na Elfu mbili  kwa siku (602,000).

" Kwetu Haya  ni mafanikio makubwa ukizingatia mradi wenyewe haujaanza kusambaza maji kwani visima hivi vilikuwa ni kwa ajili ya utafiti, kiwango cha maji kilichopatikana ni kikubwa, kilichobakia sasa ni kwa mamlaka husika na Serikali kukamilisha mipango iliyobaki ili maji haya yawafikie wananchi" Amesema.

Ameongeza kuwa chini ya mradi huo wamechimba visima 9 na kati ya hivyo visima 7 vinafanya vizuri na  2 vimeharibika na kueleza kuwa matarajio yao  ni kuona visima vitano ambavyo sasa  vimekamilika vizuri vikizalisha  lita milioni 55.

Meneja wa Mamlaka ya Maji Mkuranga mjini (MKUWASA) Muhandisi Filbert Pius akiuzungumzia mradi huo amesema kuwa utakapokamilika utawasaidia wananchi kupata maji safi na kuondoa tatizo la muda mrefu la ukosefu wa maji katika maeneo mbalimbali ya mji huo.

Amesema mahitaji ya maji katika mji huo ni makubwa kuliko uwezo wa sasa wa kuzalisha maji ambapo vyanzo vilivyopo vina uwezo wa kuzalisha lita 135,000 kwa siku  ikilinganishwa na mahitaji ya sasa ya lita 602,000 kwa siku kwa wakazi wapatao 25,847.

" Wananchi sasa watapata nafuu, tofauti kabisa na mwanzo, maji yanayozalishwa hapa ni mengi  lita 1,800,000 kwa siku hii inakidhi  mara mbili mahitaji yote ya wananchi wa mji wa Mkuranga " Amesisitiza Muhandisi Pius.

Ameiomba Serikali kuendelea kutoa fedha za kufanikisha ujenzi wa miundombinu yenye urefu wa kilometa 2 inayotarajiwa kukamilika ndani ya mwezi huu ili Mkuranga  ambao sasa ni mji wa viwanda upate  huduma ya uhakika ya maji,

Pia amesema kukamilika kwa ujenzi wa matenki makubwa ya kuhifadhia maji eneo la Mkwalia ulipo mradi huo pamoja na eneo la Kurungu kutaiwezesha hospitali ya Wilaya ya Mkuranga kupata huduma ya uhakika ya maji ambayo imekuwa kero ya muda mrefu kwa wagonjwa wanafika kupata huduma.

Meneja Uhusiano wa Jamii wa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASA) Bi.Nelly Msuya akifafanua kuhudsu mradi huo amesema unajengwa unatekelezwa na DAWASA kwa niaba ya Serikali na akifafanua kuwa maeneo yote yenye miundombinu ya maji katika wilaya ya Mkuranga yanatarajiwa kuanza kupata huduma hiyo ifikapo Oktoba mwaka huu.

Amesema mradi huo sasa uko katika hatua za majaribio na unatarajiwa kuwanufaisha wananchi wote mara  kukamilika kwa ujenzi wa miundombinu kwenye maeneo ambayo hayakuwa na mabomba ya kusambazia maji , ujenzi wa matenki makubwa ya kuhifadhia maji na kukamilika kwa  taratibu za kitaalam ili maji hayo yawafikie wananchi.

"Nachoweza kusema kwa upande wa wilayanya Mkuranga tumefika pazuri, sisi kama DAWASA watekelezaji wa miradi mbalimbali ya maji kwa niaba ya Serikali tutahakikisha kero ya maji  katika wilaya hii  na maeneo mengine inapatiwa ufumbuzi,  tumeshatoa mamlaka kwa miji na wilaya  kubuni, kusimamia  na kuendeleza miradi ya maji ili wananchi wengi zaidi wanufaike" Amesisitiza.

Aidha, amebainisha kuwa mradi wa ujenzi wa visima 8 eneo la Mkuranga umegharimu kiasi cha shilingi bilioni 7.4 na kufafanua kuwa awamu inayofuata ni kuyapeleka maji hayo yakaunganishwe na mfumo wa kusambazia maji uliopo, ujenzi, uongezaji wa matenki makubwa ya kuhifadhia maji na ununuzi wa pampu ya kusukuma maji hayo kutoka kwenye chanzo.

0 comments:

Post a Comment