SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Friday, October 24, 2014

MKUTANO WA 7 WA WADAU WA LAPF WAFUNGULIWA JIJINI ARUSHA

HOTUBA MGENI RASMI MHE. HAWA GHASIA, WAZIRI WA NCHI OFISI YA WAZIRI MKUU TAMISEMI WAKATI WA UFUNGUZI WA MKUTANO WA SABA WA WADAU WA LAPF KWENYE UKUMBI WA MIKUTANO WA AICC JIJINI ARUSHA TAREHE 23/10/2014
Mhe. Gaudensia Kabaka (mb),Waziri wa kazi na Ajira,
Mheshimiwa  Prof Hassa Mlawa, Mwenyekiti wa Bodi ya LAPF
Mhe.Magesa Mulongo,Mkuu wa Mkoa wa Arusha,
Naibu Mawaziri mlioko hapa,
Makatibu Wakuu
Waheshimiwa Wabunge Mlioko hapa,
Mwenyekiti wa Bodi ya LAPF,
Uongozi wa Mamlaka ya Udhibiti na Usimamizi wa Hifadhi ya Jamii,
Wageni waalikwa,
Mabibi na Mabwani.

Napenda kumshukuru Mwenyezimungu kwa kutujaalia afya njema na kutukutanisha sisi sote siku ya leo. Mheshimiwa mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Mfuko wa LAPF na Menejimenti kwa ujumla, napenda kuwashukuru kwa kunikaribisha siku ya leo kuwa mgeni Rasimi katika mkutano huu. Ni siku ya kipekee kwa Mfuko wa LAPF, kwani pamoja na kufanya mkutano wa saba wa wadau,mfuko unatimiza Miaka sabini tangu kuanzishwa kwake mnamo mwaka 1944.

Ndugu Wadau,

Historia tuliyoipata kuhusu Mfuko huu inatuonesha wazi kuwa Tanzania inapiga hatua katika maendeleo ya sekta ya Hifadhi ya Jamii. Sekta ya hifadhi ya Jamii inaongozwa na sera yetu ya Hifadhi ya Jamii ya mwaka 2003. Sekta hii ni pana na ipo katika mifumo mikuu miwili ambayo ni sekta iliyo rasmi na sekta hisiyo rasmi. Katika sekta rasmi tunayo mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii kama LAPF, PSPF,NSSF,GEPF,PPF na hata NHIF na taasisi nyinginezo za aina hii. Katika sekta hisiyo rasmi tunazo taratibu nyingi mbalimbali, tangu Ngazi ya familia, koo, jamii katika vijiji na mitaa kupitia vyombo kama vikoba na mifumo mingineyo, inayolenga kuifadhi na kulinda utu na heshima ya binadamu ndani ya jamii yake. Hivyo basi, Mfuko wa LAPF ni moja ya vyombo rasmi vya umma vinavyotekeleza jukumu la hifadhi ya jamii ndani ya nchi yetu. Niwapongeze si tu kwa kutimiza Miaka sabini, mkitekeleza jukumu, wajibu na dhamana mliyopewa na taifa katika hifadhi ya jamii bali pia kwa kutekeleza wajibu huo vizuri na kupata mafanikio makubwa ambayo tumekwisha ambiwa hapa.
Mheshimiwa mwenyekiti na ndugu wadau,
Mfuko huu umetoka mbali kama sote tulivyoshuhudia na pia umepitia changamoto mbalimbali lakini leo tunayaona mafanikio makubwa. Kabla ya uhuru tumesikia kuwa Bodi ya Mfuko iliundwa na machifu na baadhi ya wazungu.  Nijambo la kushukuru kwamba hata wazungu wale waliuona umuhimu wa kuwa na sekta rasimi ya hifadhi ya jamii, ambayo iliwalenga wazawa wa taifa hili. Hii inabainisha umuhimu wa sekta hii kwa nchi na dunia kwa ujumla. Hivyo, napenda kuwakumbusha wenzetu wa LAPF na mifuko mingine, kwamba dhama mliyopewa na taifa ni kubwa kwani imeshika tumaini la maisha ya baadaye ya kila mwanachama wa mfuko na pia wategemezi wao. Kufanya kwenu vizuri katika sekta hii kunamchango mkubwa katika kuboresha maisha na ustawi wa watu wa taifa hili na pia kukuza uchumi wa nchi kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha miaka 15 iliyopita na hasa baada ya Mfuko huu kuundiwa Bodi yake na kuufanya kuwa shirika la umma linalojitegemea, tumeona mafanikio mengi sana nami nichukue nafasi hii kuwashukuru na kuwapongeza sana Wenyeviti na Wajumbe wa Bodi zilizosimamia mfuko huu kwa vipindi tofauti. Lakini pia nawapongeza sana Menejimenti ya Mfuko huu kwa kasi ya ukuaji na maboresho ambayo tunayaona. Nimtambue kipekee Mzee wetu Marehemu Aloyce Bura ambaye aliongoza Mfuko huu tangu mwaka 1989 hadi 2007 alipostaafu. Kwa kweli alijitoa sana kuhakikisha mfuko huu unaimarika siku hadi siku. Namuombea Muungu aiweke roho yake mahali pema peponi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maendeleo tuliyosikia leo yanatuonesha kuwa tukidhamiria jambo litawezekana. Hii ni changamoto kwenu ninyi watendaji mlioko hapa. Kila mmoja akiweka bidii na uadilifu katika nafasi anayoifanyia kazi lazima tutaona mafanikio ambayo yatadhihirika kutokana na wananchi kuridhika na huduma wanazopata toka kwenu na kuwavuta kwa wingi zaidi kujiunga na mfumo rasmi. Lazima mjiandae kuipunguza sekta hisiyo rasmi kwa kuandikisha wanachama wengi zaidi kutoka katika eneo hilo. Kuwepo kwa vikoba, SACCOS na taasisi za aina hiyo, kunaashiria utayari wa wananchi kujiunga katika sekta ya hifadhi ya jamii. Inawezekana uchache wa wanachama kutoka katika sekta hiyo kunatokana na mifuko kuwa mbali na kuweka wigo kwa kujifunga katika sekta iliyorasmi au la mifuko haitoi elimu ya kutosha kwa umma. Ni vyema sasa, mkaongeza kasi ya kutafuta wanachama kutoka maeneo hayo ya ajira binafsi. Hii itaongeza wigo wa hifadhi ya jamii kwa kuwafikia watu wengi zaidi badala ya kuendeleza fikra ya kudhani mafanikio nikuwa na mafao mengi. Mnapofikiria kuwa na mafao mengi, hivyo hivyo mfikirie namna mtakavyo wafikia watu wengi pia.
Niwakumbushe tu kuwa kwa kweli Tanzania inaweza kufika mbali sana endapo sote kwa pamoja tukiamua kuleta mabadiliko kila mmoja mahali alipo kwa kufanyakazi kwa ujuzi na umairi na hata ubunifu pia.

Ndugu Wadau
Hivi Majuzi nilizindua fursa ya mikopo ya elimu kwa wanachama wa Mfuko huu. Kwa kweli hiki kilikuwa sio kilio cha wanachama tu bali pia hata Serikali ambayo kwa muda wote imekuwa na nia thabiti ya kuendeleza watumishi wake lakini kutokana na ufinyu wa bajeti inashindwa kufanya hivyo.
Najua mikopo ya elimu watakayopewa watumishi itawawezesha kuongeza ujuzi na hivyo wataongeza ufanisi wa kazi. Lakini pia watumishi hao wataweza kupandishwa vyeo kutokana na ufanisi wao na viwango vya elimu na matokeo yake watakuwa na mishahara mikubwa ambayo itakuja kuwapatia pensheni nzuri huko mbeleni. Hivyo jambo hili walilolianzisha LAPF kwa kweli ni zuri sana na la kuigwa na mifuko mingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti,
Huduma kama hizi ndizo zitakazowapatia imani zaidi wanachama kwenye Mfuko wao. Hata hivyo, nitoe rai kwenu kwamba wanachama wenu wanao pia wategemezi ambao wanamahitaji makubwa katika sekta hiyohiyo ya elimu ya juu. Angalieni kama inawezekana kutumia dhamana yao ndani mfuko kupata fao la elimu juu kwa wategemezi wao. Wote tunatambua ufinyu wa bajeti ya serikali katika mikopo kwa wanafunzi wanaojiunga na elimu ya juu. Hili ni soko zuri kwa mifuko kuongeza wanachama lakini pia kutoa hifadhi ya jamii inayozingatia mahitaji halisi ya watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti,
Baada ya mifuko kutoa mafao ni muhimu kwa waajiri kuhakikisha kuwa makato yanafanywa mara moja toka kwenye mishahara ya watumishi waliokopeshwa na kuwasilisha fedha hizo katika mfuko, kila mwezi bila kuchelewa. Tukumbuke kuwa wingi wa mafao ahundoi dhima ya mfuko kutoa mafao ya kisheria. Hivyo fedha hizo zisiporejeshwa wanachama tutaathirika na ni wazi mfuko utaondosha baadhi ya mafao ili uweze kumudu kutoa mafao ya kisheria. Hilo halitakuwa jambo jema hata kidogo kwani zitakuwa ni jitihada hasi za kuudhoofisha mfuko. Kamwe jambo hili halikubaliki na nilazima tulikatae na kupambana na waajiri na wale wote ambao hawafikishi mafao ya wanachama katika mfuko kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti,

Nikupongeze wewe na bodi yako, menejimenti na watumishi kwa ujumla kwa uzinduzi wa nembo mpya ambayo tumeiona na kuelezwa maana yake. Inatia faraja kwa wanachama wa mfuko kutambua kwamba nembo hii ni ishara  kuwa LAPF sasa itakwenda au kukua kwa kasi. Na kweli maendeleo tunayoona yanaonesha ukuaji wa kasi wa Mfuko huu. Naomba muendelee na kasi hiyo kamwe kurudi nyuma kwenu iwe mwiko.

Mheshimiwa Mwenyekiti,
Kama nilivyokwisha bainisha hapo awali, bado tunachangamoto kubwa  kuhakikisha huduma hii inawafikia wananchi walio wengi zaidi. Kundi tunalolishghulikia mifuko yote ni dogo sana ukilinganisha na wananchi wote wanaostahili kupata fursa kama hii. Nawaasa mamlaka ya hifadhi ya jamii na mifuko yote kufanya utafiti wa kina kuona namna nzuri zaidi ya kuwaandikisha na kuyajumuisha makundi ya waliojiajiri kwenye hifadhi hii ya jamii. Kwa kufanya hivyo mtaisaidia sana Serikali katika azma yake ya kuhakikisha kuwa  makundi mengi ndani ya jamii wakiwemo wazee wanapata hifadhi ya jamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti
Najua kuna wakati katika kutekeleza azma hii mtahitaji Serikali iingilie kati kwa kurekebisha au kutunga Sheria zitakazoongeza wigo wa wachangiaji. Nitoe rai kwenu, kuandaa  mapendekezo kupitia Wizara husika nasi tutayafanyia kazi kwa haraka ili kufikia haraka malengo yaliyopo ya kisera.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalize kwa kuwaomba waajiri na wadau mbalimbali kufanya kazi bega kwa bega na Mfuko huu kwa kutekeleza majukumu yenu ili hatimaye wanachama na wananchi kwa ujumla wanufaike na shughuli za mfuko huu. Maeneo ninayoweza kusema ni pamoja na uwekezaji, elimu kwa wanachama hasa ya maandalizi ya kustaafu, kuandikisha na kuwasilisha michango na maeneo mengine. Nafikiri mkiweka ushirikiano wa karibu kila mmoja atanufaika na mashirikiano mtakayofanya katika kutimiza azima ya taasisi yenu.

Mheshimiwa Mwenyekiti,
Nimeambiwa hapa kuwa kutokana na suala la ushindani kuna baadhi ya waajiri wanashirikiana na mifuko kuhamisha michango ya wanachama na kuipeleka katika mifuko ambayo hawajajiunga. Utaratibu huu sio mzuri na ni kinyume na Sheria, hivyo nawaasa muache na msimamie vizuri uhuru huu ambao wanachama wamepewa badala ya kuleta vuruga katika mifuko.
Mwisho kabisa nawapongeza tena mfuko wetu wa LAPF kwa kuadhimisha miaka 70 tangu kuanzishwa kwake na kusherehekea siku hii katika mwonekano mpya kama tulivyoshuhudia kwenye nembo yao. Baada ya kusema hayo naomba kusema sasa kuwa Mkutano wetu wa saba wa wadau wa LAPF umefunguliwa rasmi.

Asanteni kwa kunisikiliza.


Mhe. Waziri wa Nchi OWM - TAMISEMI

0 comments:

Post a Comment