SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Monday, March 18, 2013

WATOTO ZAIDI KUANDIKISHWA S/MSINGI KYAKA BAADA YA VODACOM KUIJENGEA VYUMBA VIPYA VYA MADARASA

  Mkuu wa Wilaya ya Misenyi Kanali Mstaafu Issa Njiku akizindua rasmi vyumba viwili vya madarasa katika shule ya Msingi Kyaka vilivyojengwa kwa msaada wa Vodacom Foundation wilayani Misenyi Mkoa wa Kagera. Vyumba hivyo vimewekewa pia jumla ya madawati tisini ikiwa ni sehemu ya Kampuni ya Vodacom kuchangia maendeleo ya elimu nchini.
  Mkuu wa Wilaya ya Misenyi Kanali Mstaafu Issa Njiku akiwasili shule ya Msingi Kyara iliyopo wilayani humo tayari kuzinduzi na kukabidhi vyumba viwili vya madarasa vilivyojengwa na Vodacom Foundation na kuviwekea jumla ya madawati tisini ili kusaidia maendeleo ya elimu. Pichani Mkuu huyo wa Wilaya akisalimiana na Meneja usimamizi wa Idara ya Mahusiano Vodacom Tanzania Lilian Kisamba.
  Mkuu wa Wilaya ya Misenyi Kanali Mstaafu Issa Njiku akifurahia jambo na wanafunzi wa shule ya Msingi Kyaka Wilayani Misenyi mkoa wa Kagera muda mfupi baada ya mkuu huyo wa wilaya kuzindua rasmi chumba hicho cha darasa kikiwa na maadwati yake kati ya vyumba viwili vilivyojengwa na Vodacom Foundation kuchangia maendeleo ya elimu Wilayani Misenyi. Wa pili kushoto ni Mkuu wa Vodacom Foundation Yessaya Mwakifulefule. Wengine ni Meneja Usimamizi  Idara ya Mawasiliano na Mahusiano ya Vodacom Tanzania,Lilian Kisamba na Meneja wa kampuni hiyo Bukoba Michael Bigambo.
Wanafunzi wa Shule ya Msingi Kyaka iliyopo Wilayani Misenyi Mkoani Kagera wakiwa katika tabasamu la matumaini ya kusoma katika mazingira yaliyoboreshwa zaidi na Vodacom Foundation kwa kuijengea shule hiyo vyumba viwili vya madarasa na kuviwekea jumla ya madawati tisini. Msaada huo ulikabidhiwa kwa uongozi wa shule na Mkuu wa Wilaya ya Misenyi Kanali Mstaafu Issa Njiku(Hayupo Pichani) katika hafla iliyohudhuriwa pia na maofisa wa Vodacom Foundation
---
Kampuni ya Mawasiliano ya Vodacom imechangia juhudi za wananchi wa Kyaka Wilayani Misenyi Mkoa wa Kagera za kuboresha na kuimarisha sekta za elimu ya msingi kwa kukabidhi vyumba viwili vya madarasa kwa shule ya msingi Kyaka vilivyojengwa kwa fedha za mfuko wa kampuni hiyo wa kusaidia jamii - Vodacom Foundation.

Kukabidhiwa kwa madarasa hayo sasa kunaiwezesha shule hiyo kuongeza uwezo wa kuandikisha wanafunzi zaidi katika jitihada za serikali za kuhamasisha na kuhuuisha jamii kuandikisha watoto wao shule za msingi ili kuendana na malengo ya milenia ya kuinua nyanja ya elimu.
 

Vodacom Foundation imeviwekea vyumba hivyo viwili vya madarasa madawati tisini ili kuhakikisha inatatua kwa mara moja changamoto mbili kuu zinazoikabili shule za msingi nchini ambazo ni vyumba vya madarasa na madawati.
 

Akiongea katika hafla ya makabidhiano iliyofanyika mwishoni mwa wiki shuleni hapo Mkuu wa Vodacom Foundation Yessaya Mwakifulefule amesema kampuni ya Vodacom itaendelea kuunga mkono juhudi za wananchi na za serikali katika kutatua matatizo ya kijamii hususan katika sekta muhimu zinazolenga maendeleo ya ustawi wa jamii ikiwemo Elimu na Afya.
 

Mwakifulefule amesema ujenzi wa vyumba hivyo viwili vya madarasa umetokana na maombi ya serikali ya kijiji na kwamba Vodacom inajisikia furaha kukamilisha ujenzi na hatimae kuvikabidhi tayari kunufaisha watoto wa Kyaka na maeneo ya jirani katika safari ya kujipatia elimu na hivyo kutengeneza maisha yao ya baadae.
 

"Tunafuraha kubwa sana leo kuwa katika eneo hili na kuwa sehemu ya maendeleo ya ustawi wa jamii za wanakijiji wa Kyaka, kazi hii ni matokeo ya dhamira ya Vodacom ya kuwa sehemu ya jamii kwa kusaidia miradi mbalimbali ya jamii."Amesema Mwakifulefule
 

Nae Mkuu wa Wilaya ya Missenyi Kanali Mstaafu Issa Njiku aliyeongoza hafla ya makabidhiano aliishukuru kampuni hiyo kwa kusaidia ufadhili wa miradi mbalmbali ya wananchi.
 
Pia alisema ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule hiyo vitaisadia Serikali kufikia lengo lake la kuboresha sekta ya elimu kutokana na kuwepo kwa changamoto kubwa katika miundombinu ya shule nyingi katika Wilaya hiyo.

Pia Kanali Njiku aliiomba Vodacom kuendelea kusaidiana na wananchi wa Wilaya hiyo ili kufikia matarajio yao ya kuwa na Sekondari mbili za elimu ya juu zitakazopokea wanafunzi wanaochaguliwa kuendelea na masomo baada ya kuhitimu kidato cha nne.
 

Kwa upande wake Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo Crotida Athanas pamoja na kuishukuru Vodacom kwa msaada huo amesema shule inapokuwa na vyumba bora vya madarasa vya aina hiyo kunaongeza morali ya kazi kwa waalimu kwa kuwa wanafunzi wanakuwa katika mazingira mazuri ya kufundishika.
 

Amesema kutokana na ukweli huo, shule itahakikisha msaada huo wa vyumba vya madarasa na madawati unatunzwa ili kutimiza malengo yanayotarajiwa kutoka kwenye msaada huo ambao ni kuiwezesha shule kuandikisha wanafunzi zaidi pamoja na kuhakikisha ufaulu kwa wanafunzi.

Mwisho
Chanzo: H@kingowi

0 comments:

Post a Comment