SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Thursday, July 29, 2010

Mafuriko yasababisha vifo vya watu 40 mashariki mwa Afghanistan



Watu wasiopungua 40 wamefariki dunia huko mashariki mwa Afghanistan na mamia ya wengine wamebaki bila ya makaazi kutokana na mvua kali zilizosababisha mafuriko katika eneo hilo. Ripoti kutoka Afghanistan zinaeleza kuwa watu 15 pia wamejeruhiwa kutokana na mafuriko hayo. Kwa mujibu wa ripoti hizo watu hao 40 wakiwemo wanawake na watoto wamefariki dunia katika majimbo ya Kapisa na Laghman. Aidha mamia ya ekari za ardhi na nyumba zimesombwa au kuharibiwa na janga hilo la kimaumbile. Kwa mujibu wa Mamlaka ya Taifa ya Udhibiti wa Majanga nchini Afghanistan, mnamo mwezi Mei, watu wasiopungua 66 walifariki dunia kutokana na mafuriko yaliyosababishwa na mvua kali zilizonyesha kwa siku kadhaa katika maeneo ya kaskazini na magharibi mwa nchi hiyo


12 wafariki dunia kwenye machafuko yanayoendelea mjini Mogadishu


Viongozi wa Serikali ya Mpito ya Somalia wamesema leo kuwa, watu wasiopungua 12 wameuawa na wengine 43 kujeruhiwa baada ya kutokea mapigano makali kati ya vikosi vya serikali na waasi wa kundi la Hizbu Islam. Ali Mussa Sheikh afisa anayeshughulikia utoaji huduma za kwanza mjini Mogadishu amesema kuwa, mapigano hayo yameanza baada ya kundi la Hizbu Islam kushambulia kambi ya vikosi vya serikali karibu na Ikulu ya Rais wa Somalia. Ali Mussa Sheikh amesema kuwa, kikosi chake kimefanikiwa kuwaokoa majeruhi 43 na kuwapeleka hospitali. Makundi ya al Shabaab na Hizbu Islam yanapambana na majeshi ya serikali yanayosaidiwa na vikosi vya Umoja wa Afrika vya kulinda amani nchini humo, kwa shabaha ya kuiangusha serikali ya mpito ya Somalia inayoongozwa na Rais Sheikh Sharif Sheikh Ahmad.

0 comments:

Post a Comment