SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Wednesday, March 23, 2016

DAWASA YATOA DARASA KWA VIONGOZI WA JUMUIYA 15 ZA WATUMIA MAJI DAR ES SALAAM, KIBAHA NA BAGAMOYO

 Meneja Uhusiano wa Jamii wa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es salaam (DAWASA) Bi.Neli Msuya akizungumza na viongozi wa Jumuiya 15 za Watumia Maji zilizojengwa chini ya mradi wa Maji Yetu uliofadhiliwa na Serikali ya Ubelgiji uliogharimu shilingi Bilioni 14.5 alipokutana nao leo jijini Dar es salaam.
Mshauri wa Ufundi wa DAWASA BTC  Mhandisi Praygod Mawalla akitoa elimu kwa viongozi wa Jumuiya 15 za Watumia Maji katika jiji la Dar es salaam namna ya kuifanya miradi wanayoisimamia ijiendeshe na kuwa endelevu kwa manufaa ya wananchi.
Mshauri wa Ufundi wa DAWASA BTC  Manjolo Kambili akitoa akitoa ufafanuzi kuhusu Programu ya za utoaji wa mafunzo kwa watumiaji wa Maji katika maeneo yenye miradi hiyo wakati wa mkutano na viongozi wa Jumuiya 15 za Watumia Maji za jiji la Dar es salaam.

Viongozi wa Jumuiya 15 za Watumia Maji zilizojengwa chini ya mradi wa Maji Yetu wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa na watendaji wa DAWASA leo jijini Dar es salaam.

Afisa Uhusiano na Jamii  wa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es salaam (DAWASA) Bi. Mecktridis Mdaku Mtaalamu kutoka akiwasisitiza viongozi wa Jumuiya 15 za Watumia Maji katika jiji la Dar es salaam kupanda miti na kuiendesha miradi katika hali ya Usafi ili kulinda afya za watumiaji wa huduma za maji.
Mkurugenzi wa Rasilimali watu na Utawala wa DAWASA Bi. Mary Ntikula akipanda mti mara baada ya mkutano na viongozi wa Jumuiya ya Watumia Maji Dar es salaam kama sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Maji na Utunzaji wa Mazingira. Kulia ni Meneja Uhusiano wa Jamii wa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es salaam (DAWASA) Bi.Neli Msuya
Baadhi ya watendaji wa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es salaam (DAWASA) wakiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Jumuiya 15 za Watumia Maji jijini Dar es salaam.


       Na. Aron Msigwa Dar es salaam.

Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es salaam (DAWASA) imewataka viongozi wa Jumuiya za watumia maji katika jiji la Dar es salaam na  baadhi ya maeneo ya Kibaha na Bagamoyo mkoani Pwani kusimamia kikamilifu mapato na matumizi ya miradi ya maji ili kuepuka migogoro inayosababishwa na matumizi mabaya ya fedha jambo linalochangia baadhi ya miradi kushindwa kujiendesha na kuwa kero kwa wananchi.

Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es salaam na Meneja Uhusiano wa Jamii wa Mamlaka hiyo Bi.Neli Msuya wakati akitoa elimu kwa viongozi hao kuhusu uendelezaji wa miradi inayosimamiwa na Jumuiya 15 za Watumia Maji zilizojengwa chini ya mradi wa Maji Yetu kwa ufadhili wa Serikali ya Ubelgiji.

Amesema DAWASA imekukutana viongozi hao kuwakumbusha wajibu walio nao katika kuhakikisha miradi wanayoisimamia inakidhi matarajio ya wananchi kwa kutoa huduma bora na kujiendesha kwa faida kwa na kuwafikia wananchi wengi zaidi.

Kwa kuzingatia idadi ya watu zaidi ya Laki mbili (200,000)  wanaohudumiwa na mradi huu kwa kupata maji safi na salama na gharama kubwa iliyotumika kuanzisha mradi huu shilingi Bilioni 14.5 ,tumeona kuna umuhimu wa kuendelea kuweka msisitizo wa uangalizi kwa kuwa miradi hii ni muhimu na iko kwa wananchi Amesisitiza.

Amewaeleza viongozi hao kuwa majukumu ya DAWASA kama mmiliki wa miundombinu ya majisafi na majitaka ni kugharamia matengenezo makubwa na kufanya uwekezaji wa kupanua miundombinu ya majisafi na majitaka jijini Dar es Salaam na maeneo yaliyoainishwa chini ya Sheria ya DAWASA Namba.20 ya Mwaka 2001.

Bi. Neli amefafanua kuwa DAWASA iliingia mkataba wa uendeshaji na Shirika la Majisafi na Majitaka Dar es salaam (DAWASCO) kutoa huduma ya uondoshaji wa majitaka katikA jiji la Dar es salaam, Kibaha na Bagamoyo mkoani Pwani.

Aidha, amesema kupitia mkataba huo,  DAWASCO huuza maji kwa wateja, kutayarisha Ankara za maji, kukusanya maduhuli, kulipia gharama za uendeshaji na kufanya matengenezo ya mfumo mzima wa usambazaji maji na uondoshaji majitaka katika maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es salaam. 

“Kupitia elimu inayotolewa leo mtagundua kuwa ninyi ni muhimu katika kuwahudumia wananchi, mtaona kuwa ninyi ni DAWASCO ndogondogo kwenye maeneo yenu kwa kuwa mnauza maji kwa wateja, mnatayarisha Ankara za maji , mnakusanya fedha za malipo ya huduma mnafanya matengenezo ya mifumo ya maji kwa wateja wenu” Amesisitiza.

Amesema kwa sasa DAWASA imewekeza kwenye miradi mikubwa na kupanua chanzo cha Maji cha Ruvu chini ambacho huzalisha lita milioni 270 kwa siku, ujenzi wa Bomba kubwa lenye urefu wa Kilometa 56 kutoka Ruvu Chini hadi matenki yaliyopo chuo Kikuu Ardhi jijini Dar es salaam.

Aidha amesema kwa upande wa Ruvu juu maboresho makubwa yamefanyika kwa kupanua mitambo ya uzalishaji ambayo sasa itazalisha lita milioni 196 kutoka milioni 82 kwa siku.

Ameongeza kuwa upande wa maeneo ya kaskazini na kusini mwa jiji la Dar es salaam kuelekea wilaya ya Mkuranga DAWASA inaendelea kuwekeza katika uchimbaji wa visima virefu vya maji na kuweka mifumo ya usambazaji wa maji ili kuwawezesha wananchi kupata maji safi na salama kwa gharama nafuu.

Kwa upande wake Mshauri wa Miradi ya Maji kutoka DAWASA BTC Bw. Manjolo Kambili amewaeleza viongozi hao kuwa wao kama viongozi wa Jumuiya za watumia maji wanatakiwa kufuata sheria na taratibu za Serikali kwa kuwa miradi hiyo ni ya Serikali.

Ameeleza kuwa jukumu la kusimamia na miradi hiyo liko kisheria hivyo viongozi hao wanapaswa kutekeleza kikamilifu majukumu yao likiwemo la kuhakikisha kuwa miradi yote inaajiri wahasibu wenye taaluma kwa lengo la kuandika na kutunza kumbukumbu za kila siku zinazohusu mapato na matumizi yao.

Naomba nisisitize katika hili, nyie mmepewa jukumu la kusimamia miradi ya maji ya Serikali, lazima mlitambue hili miradi yenu itakaguliwa na wataalamu ndio maana tuliwaomba muajiri wahasibu kwa kuwa vitabu vyenu vitakaguliwa kujua mwenendo wa mapato na matumizi yenu Amesisitiza.
Amewataka viongozi hao kuhakikisha kuwa kila mradi wa jumuiya unakuwa na akaunti ya Benki pamoja na kusimamia suala la utoaji wa risiti halali zenye nembo za jumuiya husika ili kuweka uwazi na imani wa walipiaji Ankara za maji.

Naye Afisa Uhusiano na Jamii wa Mamlaka hiyo Bi. Mecktridis Mdaku amewasisitiza viongozi hao kusimamia suala la Usafi wa mazingira, upandaji wa miti na utunzaji wa  vituo vya miradi, majengo na miundombinu ya maji ili kuwakinga wananchi dhidi ya magonjwa ya milipuko  ikiwemo. 

Ninyi kama viongozi wa Kamati za miradi ya maji lazima msimamie suala la usafi wa mazingira ili maeneo ya miradi yavutie pia kuwakinga wateja wenu na ugonjwa wa kipindupindu  Amesisitiza Bi. Mdaku.Ametoa wito kwa viongozi hao kuepuka kuyatumia majengo ya miradi ya maji ya wananchi kwa shughuli nyingine  nje ya maji ikiwemo kuhifadhi na kufanyia biashara ya mkaa.  
MWISHO.
 

0 comments:

Post a Comment