MATUKIO ya ajali za barabarani nchini
yameendelea kuteketeza maisha ya Watanzania, baada ya jana watu 12 kufa
papo hapo katika ajali iliyohusisha basi na treni katika makutano ya
reli eneo la Kiberege, wilaya Kilombero mkoani Morogoro.
Watu 40 walijeruhiwa katika ajali hiyo.Ajali hiyo, kwa mujibu wa Kamanda wa
Polisi mkoani Morogoro, Leonard Paul, ilitokea jana majira ya saa 9:15
alasiri ikihusisha basi aina ya Scania lenye namba za usajili T 725 ATD,
mali ya kampuni ya Aljabry na treni mali ya Mamlaka ya Reli ya Tanzania
na Zambia (TAZARA).Wakati basi hilo lilikuwa likitoka
Morogoro kwenda Ifaraka, treni ilikuwa inatoka Mbeya kwenda Dar es
Salaam. Kamanda Paul alisema dereva wa basi hilo ambaye hakufahamika
jina mara moja hakuwa makini wakati akivuka katika eneo hilo, hali
iliyosababisha gari alilokuwa analiendesha kugongwa kwa nyuma na treni.Alisema wote waliokufa papo hapo ni
abiria wa basi, kati yao sita wakiwa ni wanaume, wanawake wanne na
watoto wawili wenye umri wa kati ya miaka 5 hadi 6.Baadhi ya majeruhi waliondolewa eneo la
tukio na wasamaria na kukimbizwa Hospitali ya Rufaa ya Mtakatifu Francis
ya mjini Ifakara.Hata hivyo, kwa upande wa waliokufa,
watatu wametambuliwa kuwa ni Flugencia Lusangila (60) na Albeta
Lusangila (62), wakazi wa Ichonde, Mang’ula wilayani Kilombero na Joseph
Kuzwila (34) mkazi wa Dar es Salaam.Mara baada ya kusababisha ajali, dereva
alikimbia na kwamba Polisi inaendelea kumtafuta sambamba na kuchunguza
chanzo cha ajali hiyo.
0 comments:
Post a Comment