Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba
Mwenyekiti
wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba
amewataka Watanzania kutokurupuka kuipitisha Katiba Inayopendekezwa kwa
kuwa imeyaacha kando maoni yao mengi na akawataka waisome kwa makini
kabla ya kuikubali au kuikataa.
Akiwa
katika likizo ya wiki moja nyumbani kwake Bunda, Mkoa wa Mara, Jaji
Warioba alialikwa na vijana wa mji huo kupitia Jukwaa lao la Uwazi na
Fikra Yakinifu, wakiomba azungumze nao kuhusu masuala mbalimbali hasa
mchakato wa Katiba Mpya.
Katika
mkutano huo uliofanyika katika Hoteli ya Harrieth, Jaji Warioba
aliulizwa na kujibu maswali; anaionaje Katiba Inayopendekezwa na iwapo
CCM imemgeuka kwa nini asihame chama?
Akijibu
maswali hayo, Jaji Warioba alisema Katiba hiyo haina maoni yote ya
wananchi kama Bunge Maalumu lilivyojinadi, bali yamewekwa machache
ambayo hata hivyo yamo hata katika Katiba ya sasa.
Mathalan,
alisema wananchi wengi walipendekeza kiwepo kipengele cha maadili ya
viongozi ili kuwadhibiti dhidi ya vitendo viovu wanavyovifanya kwa sasa
kama ufisadi, rushwa na matumizi mabaya ya madaraka, lakini wajumbe wa
Bunge walikirekebishana hadi kikapoteza maana.(P.T)
Kwa
kufanya hivyo, alisema wajumbe hao walionyesha wanafurahishwa na hali
iliyopo ya viongozi kukosa uzalendo, uadilifu na kukosa uwajibikaji hata
kuwasababishia Watanzania maisha magumu ambayo kupitia maoni yao,
walikuwa wameyatafutia dawa kwa kupendekeza maadili yatambulike
kikatiba.
Alisema
wananchi walipendekeza muundo wa muungano wa serikali tatu ili kuondoa
matatizo yaliyopo, kupatiwa madaraka ya kuwawajibisha wabunge wao pamoja
na rais kupunguziwa madaraka, mambo ambayo yameondolewa na Bunge hilo
Maalumu.
"Kazi
yetu kama Tume ya kuandaa Katiba ya Watanzania tuliimaliza. Bunge nalo
limemaliza kazi yake japo ina upungufu. Sasa kazi imebaki kwenu wenye
Katiba; kuisoma iliyopendekezwa kwa makini kabla ya kuipigia kura,"
alisema Warioba.
Jaji
Warioba alieleza kusikitishwa na taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa
lililokuwa Bunge la Katiba, Samuel Sitta siku ya kukabidhi Katiba
Inayopendekezwa kwa Rais, kwamba Bunge hilo limeweka ndani ya katiba
hiyo asilimia 81 ya maoni ya Tume, akisema huo ni uongo mkubwa.
"Ukweli
ni kwamba wamechukua asilimia 20 tu na kutupa nje asilimia iliyobaki na
kubandika yaliyomo katika Katiba ya sasa ambayo hayawezi kuleta
mabadiliko yoyote," alisema Jaji Warioba.
Hivyo,
Jaji Warioba aliwataka Watanzania kwa umoja wao bila kujali tofauti zao
za kisiasa, dini, rangi, kabila kuhakikisha kuwa wanapata Katiba
Inayopendekezwa na kutumia muda mwingi kuisoma kabla ya kuipigia kura na
kuwa wakikurupuka watajuta siku za usoni.
Akizungumzia
hatima ya Muungano wa serikali mbili uliopo kwa sasa, Warioba alisema
hachelei kusema kwamba huenda ukakumbana na changamoto nyingi siku za
usoni iwapo wananchi watauridhia kupitia kura yao kwa vile asilimia
kubwa ya Wazanzibari hawaukubali.
"Hapa
napo kuna tatizo, Mpaka mgogoro uliopo miongoni mwa Wazanzibari
umalizwe. Wao wenyewe wanataka kuendeleza tamaduni zao ndani ya Zanzibar
wanayoitambua kama nchi huru. Sidhani kama watakubaliana," alisema
Warioba.
Kuhusu
kujitoa CCM, Jaji Warioba alisema hawezi kufanya hivyo, bali ataendelea
kuwa mwanaCCM daima kwani anaamini katika chama hicho lakini akawaponda
wanachama wenzake aliosema wanaweka masilahi binafsi mbele badala yale
ya wananchi.
"Mimi ni
mwanaCCM na nitadumu hivyo daima kwani ndicho chama ninachokiamini. Mimi
siyo mwanachama masilahi ambaye akikosa kitu fulani au akiguswa kidogo
tu anahamia chama kingine," alisema Jaji Warioba.
Chanzo:Mwananchi
0 comments:
Post a Comment