Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete.
-Imekuwa inapokea madaktari kutoka China kwa miaka 46
-Yashukuru kwa kujengewa Hospitali ya magonjwa ya moyo Muhimbili
Tanzania
imeiomba Jamhuri ya Watu wa China kuongeza idadi ya madaktari wake
inaowatuma Tanzania kama msaada kutoa huduma ya tiba kama njia ya kuzidi
kusaidia kukabiliana na upungufu wa madaktari nchini.
Aidha,
Tanzania imeishukuru China kwa kujenga hospitali kubwa inayoweza kulaza
wagonjwa 100 kwa wakati mmoja wa magonjwa ya moyo na yenye uwezo wa
kuwafanyia wagonjwa wa moyo operesheni.
Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ametoa
ombi hilo na shukurani hizo jana, Jumamosi, Oktoba 25, 2014 wakati
alipokutana na kuzungumza na Mheshimiwa Jiang Yikang, Katibu wa Chama
cha Kikomunisti cha China (CPC) cha Jimbo la Shandong, jimbo ambalo
tokea mwaka 1968 limekuwa linatuma madaktari kutoka jimbo hilo kuja
nchini kusaidia kutoa huduma ya tiba.
Rais
Kikwete ambaye yuko katika ziara rasmi ya Kiserikali katika China
amesimama kwa siku nzima katika mji mkuu wa Jimbo la Shandong wa Jinan
akiwa njiani kutoka Beijing kwenda Jimbo la Shenzhen ambako atafanya
ziara kesho, Jumapili,Oktoba 26.
Rais
Kikwete na ujumbe wake ambaye amesafiri kwa treni iendayo kasi kutoka
Beijing, amewasili kwenye Kituo cha Treni cha Jinan Magharibi kiasi cha
saa 5:53 na kupokelewa na viongozi wa Serikali na wa CPC wa Jimbo hilo,
siyo mbali na nchi jirani ya Korea kusini.
Rais Kikwete amemwambia Mheshimiwa Yikang: “Tunalishukuru
sana Jimbo la Shandong ambalo kwa miaka 46 tokea mwaka 1968 limekuwa
linatuma madaktari wake kuja Tanzania kutoa huduma ya tiba kwa msaada.
Tumepokea makundi 23 ya madaktari zaidi ya 1,000 ambao huja kila baada
ya miaka miwili. Tunalishukuru sana Jimbo hilo kwa msaada huu mkubwa.”
Ameongeza Rais Kikwete: “Lakini
bado tunazidi kuwaomba muendelee kutusaidia. Tunahitaji madaktari wengi
zaidi kwa sababu uwiano kati ya daktari na wagonjwa nchini kwetu bado
ni mkubwa. Katika mazungumzo yangu na Rais Xi Jinping jana nilitoa ombi
hili, lakini nalitoa tena hapa kwa sababu madaktari wanatoka Jimbo
hili.”
Rais
Kikwete pia amelishukuru Jimbo hilo kwa msaada uliowezesha kujengwa kwa
Hospitali ya Moyo kwenye Hospitali Kuu ya Taifa ya Muhimbili, Dar Es
Salaam. “Hospitali hii ya kisasa kabisa sasa imeanza kufanya
kazi. Imeiweka nchi yetu kwenye ngazi tofauti kabisa. Tunawashukuru
sana kwa kuendelea kuuunga mkono.”
Jimbo la
Shandong ni la tatu kwa utajiri na uchumi imara katika China ambalo pato
lake mwaka jana lilikuwa ni dola za Marekani bilioni 882.9 kiasi
kikubwa kuliko nchi nyingi za Afrika zikiwekwa kwa pamoja. Thamani ya
biashara kati ya Jimbo hilo na Tanzania kwa maka jana ilikuwa dola za
Marekani milioni 470.
Baadaye
jioni, Rais Kikwete alikutana na baadhi ya madakati waliopata kufanya
kazi katika Tanzania na akawashukuru kwa mchango wao katika maendeleo ya
huduma ya tiba nchini.
Amewaambia madaktari hao kwenye Hospitali Kuu ya Jimbo la Shandong: “Nimeomba
niwaone ili niwashukuru sana kwa kuokoa maisha ya watu wetu.
Mnashikilia nafasi ya pekee katika mioyo ya Watanzania. Kama mnavyojua
fika, madaktari wa Shandong wamekuwa wanatusaidia katika Tanzania tokea
1968 na mpaka sasa kiasi cha madaktari 1223 wametusaidia. Kuna wakati
lilikuja hapa kundi kubwa la madaktari 84 kwa wakati mmoja. Nyie mnajua
Kiswahili – Nasema asanteni sana.”
Hospitali
hiyo ni moja ya hospitali za Jimbo hilo ambazo zimekuwa zinapeleka
madaktari wake Tanzania tokea mwaka 1968. Mwaka huo, hospitali hiyo
iliweka katika kundi la madaktari waliokwenda Tanzania madaktari wake
wanne.
Katika
miaka yote 46, Hospitali hiyo imepeleka Tanzania madaktari 70 na kwa
sababu ya kazi hiyo nzuri Mei mwaka 2004, Rais Benjamin William Mkapa
aliitembelea Hospitali hiyo, akakutana na kuwashukuru madaktari
waliokuwa wametoa ujuzi wao kuokoa maisha ya Watanzania. Hospitali hiyo
iliyoanzishwa mwaka 1897, ina historia ya miaka 117 ya kutoa huduma za
tiba.
Wakati huo
huo, Rais Kikwete ametembelea Kampuni ya Kompyuta ya Inspur iliyoko
mjini Jinan na baada ya kutembelea Kampuni hiyo ameondoka mjini Jinan
kwenda mji wa Shenzhen ambako atafanya ziara ya siku mbili kuanzia
baadaye leo.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.
25 Oktoba, 2014
CHANZO: BOFAYA HAPA
0 comments:
Post a Comment