SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Thursday, March 13, 2014

MH. SAMUEL SITTA NDIYE MWENYEKITI WA KUDUMU WA BUNGE MAALUM LA KATIBA

Mwenyekiti wa Kudumu wa Bunge Maalum la Katiba mteule Mhe Samwel John Sitta akitoa neno la shukurani kwa Wajumbe kwa imani waliyoonesha kwake kwa kumchagua kwa kura nyingi kushika nafasi hiyo.

Mgombea wa nafasi ya Uenyekiti wa Kudumu wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta ameshinda nafasi hiyo kwa kura 487 dhidi ya mpinzani wake, Mhe. Hashim Rungwe aliyepaya kura 69 kati ya kura 593 zilizopigwa, na saba kuharibika katika uchaguzi uliofanyika muda mfupi uliopita Bungeni mjini Dodoma.
 Akitoa Neno la Shukrani mara baada ya kupata nafasi hiyo,Mh. Sitta amewashurukuru Wajumbe wote wa Bunge la Katiba kwa kuweza kumpa nafasi hiyo adhimu. Pia amempongeza mpinzani wake,Mh. Hashim Rungwe kwa kukubali matokeo hayo.

Sitta aja na ‘falsafa’ ya chura

Akizungumza na wajumbe ambao muda mwingi walikuwa wakimshangilia, Sitta alionekana kujiamini kabla na baada ya uchaguzi. Pia alitumia misemo lugha ya picha ikiwamo ya chura kuishi majini, akimaanisha kuwa wajumbe wamemchagua mtu mwenye uwezo, uzoefu na weledi wa kuongoza shughuli za Bunge.
"Jamani kunichagua mimi ni kama kumrejesha chura kwenye dimbwi la maji alilolizoea. Msiwe na wasiwasi ataogelea tu na ninawaahidi kuwa ikiwa kwa kudra za Mwenyezi Mungu, mtanichagua nitawatumikia kwa uaminifu, sitakubali upendeleo wa aina yoyote, nitasimamia kanuni tulizozipitisha hapa," alisema.
Aliongeza kusema: "Nitawaongoza kwa utumishi uliotukuka na uadilifu ili tupate Katiba bora, yenye viwango na kwa wakati. Nina hulka ya kuwapenda wale ninaowaongoza, kwa hiyo nitakuwa mtetezi wa shughuli mbalimbali...Ninawaahidi Watanzania kutenda haki na kuwapatia Katiba yenye viwango na kwa wakati.
Kuanzia mwaka 2005 hadi 2010, Sitta alikuwa Spika wa Bunge la Tisa la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Akiongozwa na falsafa yake ya Bunge la kasi na viwango. Pia anatajwa kufanikiwa kuliongoza Bunge hilo kwa weledi wa hali ya juu.
Kwa sababu ya mafanikio hayo, alipokuwa akiomba kura za wajumbe wa Bunge hilo, hakusita kujifananisha na chura kurudi majini.
Aidha, alisisitiza kuwa ataliongoza Bunge kwa kutumia falsafa yake ya kasi na viwango, huku akiahidi kulisimamia Bunge kwa haki na bila upendeleo kwa kundi lolote.
Matokeo ya kura
Akitangaza matokeo, Msimamizi wa Uchaguzi, Dk. Thomas Kashillilah, alisema Sitta alipata kura hizo 487 ambazo ni sawa na asimilia 86.5, kati ya kura 563 zilizopigwa.
Dk Kashillilah alisema kwamba mpinzani wa Sittta, Hashim Rungwe ambaye jana tulimwandika kimakosa kuwa anatoka NCCR- Mageuzi alipata kura 69, sawa na asilimia 12.3 ya kura zote. Alisema kura saba ziliharibika.
Moja ya mambo yaliyovuta hisia za wajumbe wengi ni hatua ya Sitta kushikana mikono ya kupongezana na Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa baada ya kumaliza kuomba kura kutoka kwa wajumbe.
Sitta na Chenge
Akitoa shukurani zake baada ya kuchaguliwa, Sitta alisema hana uhasama wowote na Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge ambaye naye awali alikuwa na nia ya kuwania nafasi hiyo kabla ya kujitoa.
"Namshukuru pia ndugu yangu Andrew Chenge ambaye watu walivumisha kwamba tulikuwa na mchuano wa uhasama ndani ya chama, jambo ambalo siyo kweli, "alisema na kuongeza;
"Mheshimiwa Andrew Chenge tuna historia ndefu sana, nikiwa Waziri wa Katiba na Sheria mwaka 1993, mimi ndiye niliyependekeza jina kwa Rais wa Awamu ya Pili, Rais Ali Hassan Mwinyi ili ateuliwe kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali." alisema.
Kwa upande wake, Chenge alisema: "Mambo yote yaliyozungumzwa na Sitta ni mambo yaliyopita, kilichopo ni kutazama kazi iliyo mbele yetu.''
Nyongeza na Beatrice Moses, Dar es Salaam
chanzo: mwananchi