SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Tuesday, April 26, 2016

SERIKALI KUBORESHA MAKAZI YA WATU WENYE ULEMAVU NA WENYE MAHITAJI MAALUM

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Watu wenye Ulemavu) Mhe Dkt. Abdallah Possi akiwasilisha hoja za masuala ya Watu wenye Ulemavu wakati wa Mkutano wa Bunge wa kujadili Bajeti ya Ofisi hiyo kwa mwaka wa fedha 2016/17 kulia ni Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana na Ajira) Mhe. Antony Mavunde tarehe 25 Aprili, 2016.
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana na Ajira) Mhe. Antony Mavunde akiwasilisha hoja zinazohusu masuala ya Kazi na Ajira wakati wa mkutano wa Bunge wa Kujadili Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2016/17 Bungeni Dodoma tarehe 25 Aprili, 2016.

Serikali imeahidi kuboresha Makazi ya watu wenye ulemavu na wenye mahitaji maalum ili kutatua changamoto wanazokabiliana nazo katika maisha yao ya kila siku.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Watu wenye Ulemavu) Mhe. Dkt Abdallah Possi wakati akichangia hoja katika Mkutano wa Bunge wa kujadili Bajeti ya Ofisi hiyo kwa mwaka wa fedha 2016/17 Bungeni mjini Dodoma.

Naibu Waziri aliwaeleza Wabunge umuhimu wa Serikali kuboresha makazi ya Watu wenye Ulemavu na wenye mahitaji maalum kwa mujibu wa matakwa ya Sheria ya watu wenye Ulemavu namba 9 ya mwaka 2010 inayoeleza haki za watu wenye Ulemavu kuboreshewa maeneo muhimu ikiwemo elimu, ajira, fursa sawa na miundombinu.

“Dhamira ya Serikali ni kuhakikiasha Watu wenye Ulemavu wanashiriki katika shughuli mbalimbali kwa kuwawekea mazingira rafiki yanayowasiaida kutekeleza majukumu yao kulingana na hali zao” Alisema Mhe.Possi.

Aidha, Serikali imefanya jitihada za awali kwa kuyatembelea makazi ya watu wenye ulemavu yakiwemo makazi ya Nunge yaliyopo wilaya ya Kigamboni mkoani Dar es salaam, Sarame Mkoani Manyara, Kituo cha Wagonjwa wa Ukoma cha Msufini mkoani Tanga pamoja na mikoa ya Arusha na Kilimanjaro na kubaini umuhimu wa kuyaangalia maeneo hayo ikiwa ni pamoja na kutatua changamoto za uvamizi wa makazi ya watu wenye mahitaji maalum.

“Makazi ya watu wenye ulemavu na wale mahitaji maalum yana changamoto nyingi ikiwemo uchakavu wa majengo, kukosa vifaa, uhaba wa wahudumu, changamoto za kifedha na uvamizi wa mara kwa mara” Alisema Naibu Waziri.

Naibu Waziri Possi alisisitiza kuwa hadi sasa Wizara hiyo imeshakubaliana na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kuangalia hatua za kuzuia uvamizi katika Makazi ya Watu wenye Ulemavu na wenye Mahitaji maalum ili kuimarisha usalama wao.

Msingi wa hoja iliyojibiwa na Naibu Waziri imetokana na michango iliyotolewa na wabunge kuhusu masuala ya Watu wenye Ulemavu kuitaka Serikali kuhakikisha inaboresha mazingira ya watu wenye ulemavu.

Maeneo  yanayoboreshwa na kutekelezwa ni pamoja na kuwaboreshea namna ya wanavyotakiwa kupata elimu bora, kukomesha mauaji ya wenye ualbino, suala la kodi na Makazi ya watu wenye ulemavu na wenye mahitaji maalum wakati wa kuchangia mjadala wa bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2016/17.

0 comments:

Post a Comment