Mstahiki
Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora Mhe. Gulam Hussein Dewji (aliyeshika
chupa ya maji) akizungumza na Waandishi wa Habari mara baada ya kutoka kuhojiwa
na Baraza la Maadili juu ya tuhuma zinazomkabili kuhusu ukiukaji wa Sheria ya
Maadili ya Viongozi wa Umma katika Ukumbi wa Karimjee, Jijini Dar es Salaam.
Shahidi
upande wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Bw. Gerald Mwaitebele
kushoto akizungumza na Mwanasheria wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa
Umma Bw. Filotheus Manula mara baada ya kutoa ushahidi wake kuhusu tuhuma za
ukiukaji wa Sheria ya Maadili zinazomkabili Meya wa Manispaa ya Tabora Mhe. Gulam Dewji mbele ya Baraza la Maadili
katika Ukumbi wa Karimjee, Jijini Dar es Salaam.
Na. Ally Mataula – Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
Meya
wa Halmashauri Manispaa ya Tabora Mhe. Gulam Hussein Dewji Remtullah
amefikishwa mbele ya Baraza la Maadili kujibu tuhuma zinazomkabili.
Akisoma
hati ya malalamiko mbele ya Mwenyekiti wa Baraza hilo Mhe. Jaji (Mst.)
Hamisi Msumi, Mwanasheria wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma
Bw. Hassan Mayunga alilieleza Baraza hilo kuwa Mlalamikiwa akiwa Meya
wa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora kwa makusudi kabisa alikiuka
Maadili ya Viongozi wa Umma kwa kukiuka kifungu cha 6(a) na (d), 12(1)
na 15 (b) vyote vya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma Na. 13 ya
mwaka 1995.
Bw.
Mayunga alilifafanulia Baraza kuwa Mhe. Gulam Hussein Dewji
analalamikiwa kwa kujinufaisha binafsi kwa kutumia fedha kiasi cha
shilingi 2,672,000/= mali ya Halmashauri ya Manispaa ya Tabora kwa ajili
ya safari ya nchini Marekani huku safari hiyo ikiwa imedhaminiwa na
kugharamiwa na Wadhamini waliomualika kutembelea nchini Marekani mnamo
Mwezi Aprili, 2011.
Pia, Mhe Gulam Dewji analalamikiwa kuvunja Sheria ya Maadili makusudi
kwa kipindi cha miaka minne yaani kuanzia mwaka 2010 hadi 2013 kwa kutoa
Tamko la uongo kwa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma huku
akijua kuwa ni kosa kufanya hivyo.
Kosa
lingine analolalamikiwa Mhe. Gulam Dewji ni kushindwa kutamka
rasilimali zake ambazo ni pamoja na viwanja Na. 100 kitalu G, 158 Kitalu
G, 637 kitalu D, 99 kitalu F, 206 kitalu C pamoja na nyumba moja
iliyopo kwenye kiwanja Na. 42 kitalu G vyote vikiwa katika Manispaa ya
Tabora.
Aidha, Mali nyingine anazodaiwa kushindwa kuzitamka Mhe. Gulam Dewji ni
pikipiki 422, duka moja, magari namba T 327 ADS Toyota Hilux, T 842 AWR
Toyota Rav4, na T 110 CMW Toyota Rav4.
Bw.
Mayunga alimaliza kumsomea hati ya malalamiko Mhe. Gulam Dewji kwa
kulieleza Baraza kuwa kwa kufanya hayo na kushindwa kutekeleza majukumu
yake kwa uadilifu ni ukiukaji wa maadili ya viongozi wa umma kwa mujibu
wa kifungu cha 6(a) na (d), 12(1) na 15(b) vyote ni vya Sheria ya
Maadili ya Viongozi wa Umma.
Aidha,
Bw. Mayunga aliliomba Baraza la Maadili lenye mamlaka ya kisheria ya
kufanya uchunguzi wa kina na kumtaka mlalamikiwa kutoa taarifa bayana
kuhusu rasilimali zake na kutoa hati na kumbukumbu ambazo ziko chini ya
udhibiti wake kuhusu rasilimali hizo kabla ya hatua nyingine kuchukuliwa
kwa mujibu wa sheria.
Naye
Shahidi wa upande wa walalamikija Bw. Gerald Mwaitebele ambaye ni
Mtumishi wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya
Magharibi - Tabora alilieleza Baraza la Maadili kuwa Ofisi ya
Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma – Kanda ya Magharibi Tabora
walipata tuhuma saba za ukiukaji wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa
Umma dhidi ya Mlalamikiwa kupitia vyombo vya habari.
Bw.
Mwaitebele aliendelea kulieleza Baraza hilo kuwa baada ya kufanya
uchunguzi wa awali walifanikiwa kupata ushahidi kwa malalamiko matatu na
mengine hawakuweza kupata ushahidi na hivyo kuamua kuyaacha.
Kwa
mujibu wa Bw. Mwaitebele tuhuma ambazo waliweza kupata uthibitisho
baada ya uchunguzi wa awali ni pamoja na kutumia madaraka vibaya kwa
kujinufaisha fedha za Halmashauri ya Manispaa ya Tabora, kutumia vibaya
madaraka kwa kujitwalia mali ambazo ni viwanja na kutoa tamko la uongo
kwa kushindwa kutaja mali zake yeye binafsi, mke pamoja na watoto wake.
Hata
hivyo Mlalamikiwa Mhe. Gulam Hussein Dewji alikana malalamiko yote
dhidi yake na Mwenyekiti wa Baraza la Maadili Mhe. Jaji (Mst.) Hamisi
Msumi aliahirisha kusikiliza shauri hilo hadi tarehe nyingine
itakayotangazwa hapo baadae.
Baraza
la Maadili ni chombo cha kisheria chini ya fungu la 26 la Sheria ya
Maadili ya Viongozi wa Umma lenye mamlaka ya kufanya uchunguzi wa kina
kuhusu malalamiko yanayohusu ukukaji wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa
Umma dhidi ya kiongozi yeyote.
Kwa
mujibu wa fungu la 26 (8) linasema kuwa katika taarifa yake, Baraza
linaweza kutoa mapendekezo kuhusu hatua za kiutawala, mashitaka ya jinai
au hatua nyingine zozote za kuchukuliwa dhidi ya kiongozi husika kwa
kadri litakavyoona inafaa.
0 comments:
Post a Comment