Afisa
Habari na Mawasiliano wa Wizara ya Viwanda na Biashara Bw.Nicodemus
Mushi (kushoto) akieleza kwa waandishi wa Habari (hawapo pichani) kuhusu
utoaji leseni za biashara chini ya sheria ya leseni za Biashara Na. 25
ya 1972 kwa Mfumo wa Kuhuisha na Kulipa ada,wakati wa mkutano
uliofanyika ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) Jijini Dar es Salaam
leo. Kulia ni Afisa Habari wa Idara ya Habari (MAELEZO) Bw. Frank
Mvungi.
Afisa
Biashara Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara Bw.Christopher Nassari
(kushoto) akifafanua jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) juu
ya mfumo huo wa ulipaji ada na kuwataka wafanyabiashara kulipa ada hizo
mapema kabla ya tarehe 31 Desemba 2013 ili kuepuka adhabu na faini,
wakati wa mkutano uliofanyika ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) Jijini
Dar es Salaam leo. Kulia ni Afisa Habari na Mawasiliano wa Wizara hiyo
Bw.Nicodemus Mushi
Baadhi ya
waandishi wa habari waliohudhuria mkutano huo katika ukumbi wa Idara ya
Habari (MAELEZO) Jijini Dar es Salaam leo.Picha na Hassan Silayo-MAELEZO
---
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA VIWANDA NA BIASHARA
1. UTANGULIZI
Serikali
ilirudisha rasmi utozaji wa ada za Leseni za biashara kupitia Sheria ya
Fedha Na.5 ya mwaka 2011. Maandalizi yamekuwa yakifanyika kutoka wakati
huo na ada zimeanza kutozwa rasmi 01/07/2013 kwa mfumo wa kuhuishwa
(Renewal).
Kutokana
na marekebisho hayo, utaratibu wa kutoa Leseni za Biashara BILA MALIPO
uliondolewa na kusitishwa na Serikali tarehe 30 Juni, 2013. Leseni za
Biashara zilizotolewa kuanzia tarehe 1 Julai, 2004 hadi 30 Juni, 2013
ambazo hazikuwa na UKOMO zinatakiwa kupelekwa kwenye Mamlaka zilizotoa
Leseni hizo, ili zihuishwe na kulipiwa ada kwa madhumuni ya kuongeza
mapato kwa Serikali.
Kila
mfanyabishara mwenye Leseni ya Biashara anapaswa kujaza Fomu ya Maombi
ya Leseni ya Biashara na kuambatisha Leseni ya Biashara aliyonayo na
kuiwasilisha katika Mamlaka husika, kwa ajili ya kuhuisha na kulipia
ada. Maombi yapelekwe katika Mamlaka iliyotoa Leseni husika. Kwa Leseni
za Biashara za kundi “A” kama ilivyoainishwa kwenye Fomu ya Maombi ya
Leseni ya Biashara TFN Na. 211ya 2004 hutolewa na Wizara ya Viwanda na
Biashara. Maombi hayo yawasilishwe katika Ofisi za Wizara ya Viwanda
na Biashara zilizopo Barabara ya Sokoine Jengo la NSSF-“Water front”,
Ghorofa ya Nne chumba Na. 416. Kwa wale Wafanyabiashara wa Kundi “B”
kama ilivyoainishwa kwenye Fomu ya Maombi ya Leseni ya Biashara TFN Na.
211ya 2004 wafike Ofisi za Halmashauri za Majiji, Manispaa na Wilaya
zilizo katika maeneo yao, watapata huduma kutoka kwa Maafisa Biashara wa
Mamlaka za Serikali za Mitaa.
2. UTARATIBU WA KUFUATA ILI KUFANIKISHA ZOEZI NA KUPATA HUDUMA KWA HARAKA
- Kwa wafanyabiashara wa Kundi “A” wajaze Fomu ya Maombi ya Leseni za Biashara (fomu inapatikana katika tovuti ya Wizara sehemu ya Marketing Sector (www.mit.go.tz) au fika Wizarani NSSF-Waterfront ghorofa ya 4 chumba Na. 416, Kwa Wafanyabiashara wa Kundi “B” wawasilishe maombi Ofisi za Halmashauri za Majiji, Manispaa na Wilaya zilizo katika maeneo yao;
- Waambatishe Leseni za Biashara za kudumu walizonazo na kuwasilisha kwenye Mamlaka husika kama ilivyoainishwa hapo juu;
- Kwa wafanyabiashara wa Kundi “A” wafanye malipo kupitia Benki ya CRDB mahali popote kwa kutumia Account Number 0150413356300; jina Revenue Collection Trading License-MIT. Wafanyabiashara wa Kundi “B” wataelekezwa Benki ya kulipia na Halmashauri zao;
- Kwa wafanyabiashara wa Kundi “A” wawasilishe “pay slip” ya Benki ghorofa ya Mezanine (NSSF-WaterFront) kwaajili ya risiti ya Serikali, Wafanyabiashara wa Kundi “B” wataelekezwa Ofisi ya kuwasilisha ili wapewe reisiti ya Serikali-Mweka Hazina wa Halmashauri;
- Kwa wafanyabiashara wa Kundi “A” wawasilishe Fomu ya Maombi ya Leseni ya Biashara, Leseni ya Biashara na risiti ya malipo ghorofa ya 4 kwa ajili ya kuandikiwa Leseni ya Biashara, Wafanyabiashara wa Kundi “B” wataelekezwa ofisi ya kupeleka na kuandikiwa Leseni ya Biashara ofisi za Biashara za Halmashauri.
Waombaji
wapya wa Leseni za Biashara mnapaswa kujaza fomu ya maombi ya Leseni
za Biashara na kuambatisha nyaraka kama inavyojieleza katika fomu ya
maombi na kufuata hatua ya 1 hadi 5 kama ilivyoelezwa hapo juu.
Mnashauriwa
kuhuisha na kulipia ada Leseni za Biashara mapema kabla ya tarehe 31
Desemba, 2013 ambapo adhabu na faini kwa wafanyabiashra watakaochelewa
kuhuisha (Renew) itaanza kutolewa tarehe 1 Januari, 2014.
- TAHADHARI
Wafanyabiashara
mnatadharishwa kuwa hapa mjini kuna mawakala wasio waaminifu maarufu
kwa jina la VISHOKA. Mnashauriwa kuwaepuka na muweke utaratibu wa
kufuatilia Leseni za Biashara zenu wenyewe.
Kwa
wale ambao, wameshaletewa Leseni za Biashara na mawakala waliowatuma
mnashauriwa kwenda kwenye Mamlaka iliyotoa Leseni husika kwa ajili ya
kufanya uhakiki kwa kuwa imebainika kuwa kuna baadhi ya wafanyabiashara
wanaofanya biashara kwa kutumia Leseni batili (Feki)
TAFADHALI FIKA NA KUFANYA UHAKIKI KWA FAIDA YA BIASHARA YAKO.
MAELEZO ZAIDI YANAWEZA KUPATIKANA PIA KWA KUTUMIA ANUANI IFUATAYO:
Katibu Mkuu,
Wizara ya Viwanda na Biashara,
S. L. P. 9503,
Simu Na-+255-22-2127897/8,
Fax: +255-22-2125832
Website – www.psmit.go.tz
DAR ES SALAAM.
WIZARA YAVIWANDA NA BIASHARA
0 comments:
Post a Comment