Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.
Jakaya Mrisho Kikwete akiwa kwenye mkutano wa ILO Geneva, Uswiss.
*************************************
Upungufu wa
ajira hususan miongoni mwa vijana ni changamoto kubwa kwa nchi
zinazoendelea kwa sababu ya uchumi wake kuwa mdogo na kukua polepole.
Rais Jakaya
Mrisho Kikwete ameyasema hayo Jumatano wiki hii (15 Juni, 2011) wakati
wa hotuba yake katika kikao cha 100 cha Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Shirika
la Kazi Duniani (ILO) katika makao makuu ya shirika hilo mjini Geneva, Uswiss.
“Tunahitaji
kutatua tatizo la ajira ambalo linaongezeka, hasa kwa vijana katika
nchi zinazoendelea,ili kulitatua kwa umakini zaidi juhudi za pamoja
zinahitajika baina ya serikali, jumuiya za wafanyabiashara wa kitaifa
na kimataifa, mashirika ya kiraia na washirika wetu wa kimaendeleo”, Amesisitiza na kufafanua kuwa “ Kwa ushirikiano baina ya pande zote kasi ya kuongeza na kutengeneza ajira inahitajika katika nchi zinazoendelea”. Rais Amesema.
Mara baada
ya kuhutubia mkutano huo, Rais pia alipata nafasi ya kuzungumza na
viongozi na wawakilishi wa nchi za Afrika waliohudhuria Mkutano huo.
Alisisitiza
kuwa nchi za Afrika zinakabiliwa na changamoto ya ajira na kwamba kwa
pamoja ushirikiano wa kikanda unahitajika kupitia jumuiya mbalimbali za
kiuchumi barani Afrika kama vile Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC), Soko la pamoja la Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika (COMESA), Jumuiya ya Uchumi ya Nchi za Afrika Magharibi (ECOWAS) na nyingine ambazo kwa pamoja zinaweza kupanua ajira na kuongeza kasi ya kukua kwa uchumi kwa bara la Afrika.
Shirika la
Kazi Duniani ni shirika ambalo huendesha shughuli zake kwa kanuni ya
utatu ambapo hujumuisha viongozi wa kiserikali, viongozi wa vyama vya
waajiri na vyama vya wafanyakazi duniani na ujumbe wa kila nchi
huhudhuria vikao hivi kwa kuzingatia utatu huu.
Katika
hatua nyingine Rais Kikwete amewaeleza mabalozi, viongozi wa vyama vya
wafanyakazi na waajiri barani Afrika juu ya makubaliano makuu matatu ya
jumuiya tatu za EAC, COMESA na SADC katika
kikao chao kilichofanyika mwishoni mwa juma lililopita nchini Afrika ya
Kusini, kuwa viongozi hao waliazimia kwa pamoja kuunda muungano mkubwa
wa soko huru (Free Trade Area) kwa kipindi cha miaka mitatu ijayo.
Maeneo hayo ni kukuza masoko baina ya nchi hizi, miundo mbinu na nishati.
Rais amesema maendeleo haya yanalenga katika kukuza uchumi na hatimaye kuongeza na kutengeneza ajira zaidi.
Rais
Kikwete pia ametoa changamoto kwa wananchi wa Afrika kuacha kuwa
wanyonge na kudharau maendeleo yaliyokwisha patikana katika nchi zao,
amesema inasikitisha kuona Waafrika wanaongea kwa kujidharau na
kujidhalilisha wenyewe bila hata kuona kufanya hivyo ni kujikosea
binafsi.
“Tunahitaji
kuwa wazalendo na pia kuwa na matumaini na bara letu na juhudi zetu
katika kujiletea maendeleo na sio kujidharau wenyewe” Rais amewaasa wawakilishi wa Afrika.
Rais Kikwete amerejea jijini Dar-Es-Salaam jana (16 Juni 2011) jioni.
Imetolewa na Premi Kibanga,
Mwandishi wa Habari wa Rais Msaidizi.
Geneva-Uswiss.
17 Juni, 2011
0 comments:
Post a Comment