SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Thursday, May 27, 2010

'Muuaji' aomba nauli atoroke Dar es Salaam

KUNA taarifa kwamba, polisi wamemkamata mlinzi wa sekondari ya Aboud Jumbe, Kigamboni, Shemsa Mpelela (22), anayetuhumiwa kuchoma moto nyumba na kuua watu watano wa familia moja.
Sambamba na kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo wa mauaji, jana vilio vilitawala kutoka kwa mamia ya watu waliohudhuria maziko ya watu hao watano yaliyofanyika Tungi, Kigamboni, Dar es Salaam.
Walioteketea kwa moto wakiwa katika nyumba yao yenye chumba kimoja ni baba mwenye nyumba John Onesmo (32) ambaye ni mfanyabiashara wa samaki eneo la Feri, Catherine Jackson (25) anayefanya biashara ndogo, watoto wao Oliver (2) na Joyce John (5) na Esther Mugulu (20) ambaye ni mdogo wa Catherine, aliyekuwa na uhusiano wa kimapenzi na Shemsa na kutokana na ugomvi baina yao, alidaiwa kuchoma nyumba hiyo ya chumba kimoja.
Taarifa zilizopatikana jana eneo la msiba zilidai kuwa juzi Shemsa alikwenda kwa kaka yake eneo la Kigamboni, Kisiwani, kuomba nauli ili aondoke Dar es Salaam ndipo watu walipomwona na kutoa taarifa Polisi ambao walimkamata huku umati wa watu ukishuhudia.
“Watu walimwona mtuhumiwa na kutoa taarifa Polisi na wao kwenda kumkamata na polisi waliwahi na kumkuta eneo la Sido Kigamboni saa 4 asubuhi huku wananchi tukishuhudia,” alisema binamu wa John, Majuto Daudi.
Habari hizo zilizozagaa eneo hilo la msiba, zilibainisha kuwa mbali na kukamatwa kwa Shemsa, pia Polisi iliwakamata marafiki wawili wa mtuhumiwa huyo, akiwamo anayedaiwa kushirikiana naye kuchoma moto nyumba hiyo na kusababisha vifo.
Inadaiwa Jumatatu rafiki wa mtuhumiwa ambaye jina lake halikufahamika, aliropokwa kijiweni kuwa mtuhumiwa huyo siku ya tukio alikwenda nyumbani kwa John na kumtaka amtoe mpenzi wake, lakini John licha ya kukubali kuwapatanisha alikataa kumtoa akidai kesi imeshafikishwa polisi na ndipo Shemsa alipokasirishwa na usiku wake kuamua kuchoma nyumba.
“Rafiki yake alisema mtuhumiwa alikuwa akinunua lita moja moja za petroli na zilipofika lita 10 alimwomba rafiki yake amsindikize, lakini rafiki huyo hakujua tendo alilokuwa anakwenda kufanya na ndipo aliposhangazwa kuona mwenzake akichoma nyumba na wakaondoka eneo la tukio haraka na kukaa mbali huku wakishuhudia nyumba inavyoteketea aliposema hivyo, polisi jamii walimkamata na kuita askari Polisi,” alidai Daudi.
Mwenzake mwingine aliyekamatwa na Polisi ambaye ni mchunga ng’ombe anadaiwa kumficha Shemsa sehemu anakoishi Kigamboni tangu Ijumaa alivyomchoma kisu mchumba wake.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Temeke, David Misime, alipoulizwa, hakupinga wala kukubali kama mtuhumiwa huyo amekamatwa.
“Siwezi kuzungumza na mwandishi kwa njia ya simu, taarifa zangu nazitoa kwa maandishi tu ukitaka taarifa zangu njoo ofisini nikupe kwa maandishi,” alisema.
Hata alipoombwa na mwandishi kutokana na muda ulivyokuwa umekwenda na foleni barabarani kuwa kubwa, hivyo mwandishi angechelewa kufika ofisini kwake, Kamanda huyo alikataa na kukata simu.
Gazeti hili lilipomtafuta Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu, Suleiman Kova, hakupatikana hadi tunakwenda mitamboni.
Katika hatua nyingine, vilio vya umati wa waombolezaji jana waliofurika nyumbani kwa baba yake John, Onesmo Magandu, kulipofanyika maziko, vilisikika na kulifanya eneo la mtaa huo kuzizima huku watu wakimlaani mtuhumiwa aliyefanya mauaji hayo.
Miili ya marehemu iliwasili nyumbani kwa Onesmo saa 9 alasiri na sala ya kuwaombea iliongozwa na Mchungaji wa Kanisa la Anglikana wa Tungi, Obed Ntigogozwa na baadaye majeneza yote matano yalipelekwa kuzikwa eneo la makaburi la Vijibweni.
Hata hivyo miili ya marehemu hao haikuoneshwa, kutokana na kuharibika kwa moto na watu kutopita mbele ya majeneza hayo kutoa heshima za mwisho.
Akitoa mahubiri wakati wa sala ya kuwaombea marehemu, Mchungaji Ntigogozwa, alisema tukio hilo linaonesha watu walivyobadilika na kugeuka wanyama, matukio ambayo hutokea siku za mwisho wa Dunia.
“Tukio hili litufanye tuone tunaishi siku za mwisho, tunaishi na watu ambao si watu ingawa kwa mwonekano utafikiri ni watu … viongozi nao wanapotaka uongozi wanakwenda kwa waganga na kuua albino, sasa hivi waganga wanaharibu Taifa na tunakuwa na viongozi mbumbumbu. Waganga wakamatwe kama majambazi,” alisema.
Katibu wa CCM wa Wilaya ya Temeke, Saad Kusilawe, aliyehudhuria maziko hayo akifuatana na Mwenyekiti wa chama hicho wilayani humo na Diwani wa Vijibweni, Lucy Kanyopa, aliwataka wananchi kuepuka dhana ya kujichukulia sheria mkononi. Chama hicho kilitoa rambirambi ya Sh 100,000.
Shemsa anadaiwa kuchoma nyumba ya John na familia yake usiku wa kuamkia Jumatatu wiki hii na kuua watu wote
Na Maulid Ahmed-Habari Leo
                            ****************************
Image
Waombolezaji wakiwa kwenye ibada Tungi Kigamboni kuwaombea watu watano wa familia moja waliokufa kwa kuchomwa moto ndani ya nyumba, Kigamboni, Dar es Salaam. (Picha na Mroki Mroki).

0 comments:

Post a Comment