SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Thursday, May 27, 2010

Mtoto aliyetaka kulipua ubalozi afikishwa kortini

MTOTO Nassib Mpamka (15), anayetuhumiwa kufanya jaribio la kulipua Ubalozi wa Marekani Dar es Salaam, amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam.
Mpamka alifikishwa mahakamani hapo saa mbili asubuhi na kuwekwa chumba cha maulizo akiwa chini ya ulinzi wa maofisa wa Polisi.
Haikufahamika anakabiliwa na mashitaka gani kwa kuwa maofisa wa mahakama walidai jalada lake lilihamishiwa mahakama ya watoto na mashauri yake hayaruhusiwi kuripotiwa katika vyombo vya habari.
Kwa kawaida mahakama hiyo ya watoto hufanya shughuli zake asubuhi na kumalizika kabla ya saa tatu ili kuruhusu watoto hao kuhudhuria masomo.
Ofisa mmoja wa Polisi aliyevaa nguo za kiraia, alionekana akimchukua Mpamka kutoka chumba cha maulizo kilichopo katika mahakama ya kawaida na kumpeleka katika chumba kimoja kilichopo katika jengo ambalo mahakama ya watoto hufanyia shughuli zake.
Alipotoka katika chumba hicho, alirudishwa tena katika mahakama ya kawaida na taarifa kutoka ndani ya mahakama hiyo zilidai kuwa, Mpamka alikuwa akitafutiwa hakimu wa kusikiliza mashitaka yake baada ya kukosa hakimu katika mahakama ya watoto ambako ndiko jalada lake liliko.
Haikuweza kufahamika mara moja kama alisomewa mashitaka hayo au la, kwa kuwa hakuna aliyekuwa tayari kueleza kinachoendelea kuhusu mtuhumiwa huyo.
Kwa kawaida kesi za watoto zinaendeshwa kwa usiri na si wazi kama zilivyo kesi za kawaida. Taarifa kutoka chanzo chetu ndani ya Polisi zilieleza kuwa alipelekwa katika mahabusu ya watoto iliyoko Upanga, Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa madai ya Polisi, Mpanga alifanya jaribio hilo baada ya kuhamasika na mahubiri ya shehe wa msikiti wa Mtambani na kwamba wazo la kulipua ubalozi huo alikuwa nalo tangu mwishoni mwa mwaka jana.
Kaimu Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai, Naibu Kamishna wa Polisi, Peter Kivuyo alikaririwa na vyombo vya habari akisema mtuhumiwa huyo alibainisha kuwa shehe huyo ambaye mpaka sasa hajatajwa jina, alikuwa akihubiri mara kwa mara kuhusu vitendo vya majeshi ya Marekani kuwaua Waislamu katika nchi mbalimbali duniani.
Kivuyo alisema wanahojiwa watuhumiwa wawili, yaani Mpamka na mwenzake Amani Thomas (15), ambaye pia ni mwanafunzi wa kidato cha pili katika shule ya sekondari Biafra.
Mei 16 saa 2:30 usiku, Mpamka alidaiwa kufika katika viunga vya ubalozi huo katika eneo ambalo linaegeshwa magari ya kubebea maji na kurusha chupa iliyokuwa imejazwa mafuta ya taa na kuwekwa utambi kwa lengo la kulipua magari hayo.
Kutokana na juhudi za walinzi wa ubalozi huo waliokuwa kazini, walifanikiwa kumkamata mtuhumiwa huyo na kumfikisha Polisi kwa mahojiano zaidi.
habari Leo.

0 comments:

Post a Comment