SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Tuesday, June 21, 2016

Mchezo wa Shuga wabadilisha tabia za vijana

Mratibu wa mradi wa Shuga akijibu maswali yaliyokua yanaulizwa na kikundi cha wasikilizaji cha Iwawa- Makete mkoani Njombe.
Wakionyesha furaha zao baada ya kuelewa mada ya siku ukihusianisha na maisha yao ya kila siku
Mwezeshaji wa kikundi cha wasikilizaji wa Kihesa, Manispaa ya Iringa mjini akitimiza jukumu lake la kuelimisha wenzake na kuwawezesha kushiriki katika majadiliano baada ya kusikiliza kipindi
Vijana wa Iringa wakionyesha nyuso zenye furaha baada ya kuongeza uelewa kupitia majadiliano baada ya kipindi cha saba cha mfululizo wa vipindi vya Shuga
 Kikundi cha wasikilizaji kutoka kijiji cha Kabanga, Kyela wakifurahia uelewa walioupata juu ya kukabiliana na changamoto zinazowakumba katika maisha yao
Kikundi cha wasikilizaji Jitambue 1 kutoka wilaya ya Kyela mkoani Mbeya wakijadiliana sehemu ya saba ya mfululizo wa vipindi vya mchezo wa redio wa Shuga.
Wakina mama wakifuatilia mjadala kuhusu kujitambua na namna ya kujikinga na Virusi vya UKIMWI pamoja 
 Mwana kikundi wa AMKA- Njombe vijijini akiwashirikisha wanakikundi wenzie uzoefu wake katika kukabiliana na changamoto za kutakwa kimapenzi na wanaume waliomzidi umri
Mwanachama ambaye amekua baba katika umri wa miaka 19 akionyesha shukrani zake kwa vipindi vya Shuga kwa kumuwezesha kujitambua, kwenda kupima afya yake na kujiwekea malengo ya kujilinda yeye, mama pamoja na mtoto dhidi ya maambukizi ya VVU
Tunajitambua, Tunajipenda na Tunajilinda na VVU. Tumepima - Kikundi cha AMKA kutoka Njombe
UGONJWA  wa UKIMWI umekuwa janga kubwa sana duniani huku wadau mbalimbali wakiendelea kutoa elimu na kuhamasisha katika kuanzisha programu mbalimbali za kubadilisha tabia chanya kwa jamii.
Akizungumza mwishoni mwa wiki, Mratibu wa mchezo wa redio wa Shuga alisema  tayari wameanzisha programu mbalimbali za vipindi vinavyolenga kuelimisha jamii hususani  vijana juu ya  maambukizi ya Virusi vya ukosefu wa kinga mwilini (UKIMWI), usawa wa jinsia, kufanya maamuzi sahihi, matumizi sahihi ya kinga na kuepukana na msongo rika.
Alisema mfululizo huu wa mchezo wa redio wa Shuga unawalenga zaidi vijana hususan wasichana, kwa kuangalia mtazamo wao, matarajio  pamoja na changamoto wanazopitia kwa  njia sahihi za kukabiliana na changamoto ili kutimiza malengo yao. 

"Mchezo wa redio wa Shuga ulianzishwa mnamo mwaka 2014 kwa ushirikiano kati ya MTV, HIV and AIDS Free Generation, Shirika la TACAIDS pamoja na UNICEF. Baada ya mafanikio makubwa msimu wa kwanza, TACAIDS na UNICEF pamoja na wadau wengine waliamua kupanua wigo wa program hii kwa kuandaa vipindi zaidi ili kuimarisha tabia chanya zilizojengwa katika msimu wa kwanza wa vipindi vya Shuga," alisema Laizer 

Alisema mfululizo wa vipindi vya redio vya Shuga awamu ya pili vilianza kupitia redio mbalimbali nchini kuanzia wiki ya pili ya mwezi wa nne 2016 kwa lengo la kuendeleza elimu ya masula ya UKIMWI.
"Katika kuboresha utoaji elimu kuhusiana na maudhui ya vipindi, kampuni ya True Vision Production imefanya ufuatiliaji wa utekelezaji wa awamu ya pili ya  mfululizo wa vipindi vya redio vya Shuga katika kuhakikisha jamii inakuwa na uelewa juu ya masuala hayo." alisema Laizer. "Kwa sasa, vituo mbalimbali vya redio vinarusha sehemu ya nane ya mfululizo wa vipindi vya Shuga." Aliongezea Laizer. 
Alisema Matokeo ya mradi huu yameanza kuonekana na vijana ambao ni walengwa wakuu wametoa ushuhuda wao kuhusiana na kipindi hicho cha Shuga na kusema kuwa klipindi kimewaletea mabadiliko makubwa.
‘Vijana tunajitambua, tumehamasika kwenda kupima afya zetu, tunajua njia sahihi za kujilinda na magonjwa ya zinaa na pia tunajiwekea mipango endelevu," alisema Abbas Boniphace, mmoja wa wasikilizaji wa kipindi cha Shuga kutoka Njombe
"Ningepata nafasi ya kusikia Shuga mapema nisingepata ujauzito katika umri mdogo. Sikua na uelewa wakati huo, sasa najitambua, nimepima na najilinda, siwezi kudanganyika" alisema Herieth kutoka Njombe.
"Wazazi huogopa kutuambia ukweli juu ya maswala yahusuyo VVU na UKIMWI ila Shuga inaelezea kwa uwazi zaidi." Alisema Shamila Juma, mwana kikundi cha wasikilizaji wa vipindi vya Shuga

0 comments:

Post a Comment