SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Wednesday, May 8, 2013

WANAWAKE UNGANENI KUPIGANIA KATIBA BORA ZAIDI - KAIRUKI

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Angellah Jasmine Kairuki, akisalimiana na Mkurugenzi wa TGNP, Bi. Usu Mallya.
Akina mama wakiwa na mabango ya uzinduzi wa ilani hiyo.
Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Angellah Jasmine Kairuki, akikata utepe kuashiria uzinduzi huo.
Wanaume nao hawakuwa nyuma kuwaunga mkono akina mama.
****

Na Walusanga Ndaki
WANAWAKE nchini wametakiwa kuacha tofauti zao za kiitikadi, kisiasa na kidini ili wafanikishe kupatikana kwa  katiba mpya ambayo itawakilisha na kupigania maslahi yao kwa jumla.
Hayo yalisemwa na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Angellah Jasmine Kairuki, wakati akizindua Ilani ya Madai ya Wanawake nchini katika Katiba Mpya kwenye  viwanja vya makao makuu ya Mtandao wa Jinsia nchini (TGNP), Mabibo, jijini Dar es Salaam leo.
Kairuki pia aliwaasa wanawake waliokusanyika katika hafla hiyo kukataa kutumiwa na wanasiasa ambao wanaweza kuwayumbisha na kuwaondoa katika mapambano ya kupigania katiba ambayo itatia maanani mahitaji yao.
“Matatizo ya wanawake nchini yanafanana kila mahali na katika kila jamii, hivyo unganeni kupigania maslahi yenu na si ya kikundi chochote.  Na nawahakikishia kwamba serikali itaunga mkono  kila mnachotaka kukifanya ikiwa pamoja na kupigania kupatikana katiba mpya,” alisema.
Akiipongeza TGNP kwa kusimamia harakati za ukombozi wa wanawake na haki za binadamu, Kairuki  alisema kuzinduliwa kwa Ilani hiyo ambayo kama matakwa yake yataingia katika katiba mpya, utakuwa ni ushindi katika harakati za kuleta usawa wa kijinsia na kujenga jamii huru nchini kwa vile minyororo inayomfunga mwanamke ikikatwa, jamii nzima itakuwa huru.
Alipongeza hatua kadhaa zilizopigwa nchini katika kumkomboa mwanamke na kumwezesha kushiriki kwa kiasi fulani katika shughuli za kiuchumi na uzalishaji mali.
“Hata hivyo, ongezeko hili ni dogo mno likilinganishwa na ukubwa wa tatizo lenyewe na historia ya muda mrefu,” alisisitiza.
Naibu waziri huyo alikumbushia jinsi haki za wanawake zikiwemo za kupiga kura zilivyokuwa zimepuuzwa karibu dunia nzima ambapo kwa nchi za Ulaya zilitambuliwa mnamo karne ya 20, na si kabla ya hapo.
“Mbali na kuwa wanawake ni asilimia 50 duniani, pia ni asilimia 40 ya nguvu kazi duniani.  Katika Afrika, wanawake huzalisha asilimia 80 ya chakula lakini wanamiliki asilimia 1 tu ya mali,” alisisitiza na kuongeza kwamba licha ya kukabiliwa na matatizo hayo, mwanamke mmoja katika kila wanawake 10 amekutana na vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia.
Wakati huohuo, akimkaribisha waziri huyo kuzungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa TGNP Mtandao, Bi  Usu Mallya, alisema Ilani hiyo ina malengo manne ambayo ni pamoja na kutambuliwa kwa madai ya wanawake katika mchakato mzima wa kuandika katiba mpya.
Lengo la pili alisema ni kutaka kuwawezesha wanawake wote, kama si wengi zaidi, kushiriki katika mchakato wa kuhakikisha madai yao yanajumuishwa katika katiba.  Na lengo la tatu alisema ni kuweka mkakati wa kuhakikisha serikali husika inawajibika katika kuyatekeleza madai  ya wanawake yatakayokuwemo katika katiba mpya.
Na lengo la nne alisema ni kujenga nguvu ya pamoja ya wanawake wote ambayo itawawezesha kupigania kwa pamoja malengo na maslahi yao bila kubaguana kwa misingi yoyote ile kwa vile matatizo yao katika jamii yanafahamika.

0 comments:

Post a Comment