SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Wednesday, April 6, 2011

Babu Wa Loliondo Awafunda Wanandoa

NA SHAABAN MDOE, LOLIONDOLinkMchungaji mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Ambilikile Masapila, amewataka watu wanaoishi na virusi vya ukimwi wanaokwenda kupata tiba waende na wenzi wao.
Akitumia kipaza sauti, Masapila ‘Babu’ alitoa agizo hilo jana asubuhi nyumbani kwake Samunge, Loliondo, wilayani Ngorongoro, kabla ya kuanza kutoa tiba kwa umati uliofika kupata ‘kikombe’.
Kwa mujibu wa Masapila, amekuwa akitoa tiba nusunusu, hivyo kusababisha maambukizi mapya ya virusi vya ukimwi kuendelea. Alisema tangu kuanza kwa tiba hiyo, watu wengi walioathirika bila kutaja matatizo yao wamekuwa wakifika nyumbani kwake kupata tiba ya maradhi nyemelezi pasipo kufuatana na wenza wao
.
“Jamani ninyi mliopo hapa nendeni mkawaambie wale wasiokuwepo kuwa waje na wenza wao. Bila kufanya hivyo tiba haitakuwa na maana, wewe msafi halafu unashirikiana na mwenza wako asiye msafi hilo haliwezekani,” alisema.
Alisema anachofanya ni kutoa dawa yenye mkono wa Mungu kutibu maradhi yasiyo na tiba, na si magonjwa sugu ambayo mengi yanatibika.
Mchungaji Masapila alisema tiba hiyo ni kwa ajili ya kutibu na si kinga kama inavyozungumzwa na baadhi ya watu, hivyo kufanya umati kufika nyumbani kwake bila kufuatana na wenza wao.
Kutokana na dhana hiyo potofu, alisema watu hao wamekuwa wakipata tiba bila wenza wao na baadae kurudi kwao na kuendelea kushiriki nao tendo la ndoa wakiwa wameathirika.
“Natoa tiba ya ukimwi, saratani, moyo na kisukari, kamwe dawa hii si kinga, hivyo ukirejea matendo maovu na waathirika lazima utapata maambukizi, waambieni wenzenu waje na wenza wao,” alisema Babu.
Alisema agizo hilo linawahusu pia wenye wenza zaidi ya mmoja, waliofunga au kutofunga ndoa, kwa kuwa wanashiriki nao tendo la ndoa jambo litakalowafanya wapate maambukizi mapya.
Masapila alisema endapo watu watafuata agizo hilo, ni wazi maambukizi mapya ya virusi vya ukimwi yatakwisha.
Aliwataka wagonjwa wa ukimwi kupima afya zao siku saba baada ya kupata tiba, akisema wataona ongezeko la chembe za CD4, ambazo hufanya kazi ya kupambana na maradhi mwilini.
Kwa mujibu wa Masapila, mgonjwa anatakiwa kupima tena afya yake baada ya miezi mitatu na ataona tofauti kubwa ya CD4.
BOFYA HAPA

0 comments:

Post a Comment