SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Tuesday, July 6, 2010


Mashabiki wawalaki Black Stars Ghana
Timu ya soka ya taifa ya Ghana imerejea nyumbani kutoka kwenye Kombe la Dunia Afrika Kusini ikiwa imekaribishwa na mashabiki wenye furaha kupita kiasi.
Maelfu ya mashabiki waliokuwa wakiimba na kucheza waliwakaribisha wachezaji hao-wanaojulikana kama Black Stars-kwenye uwanja wa ndege wa Accra.
Naibu waziri wa michezo Nii Nortey Duah amewaambia wachezaji, " Mmeipeperusha bendera ya Ghana ipasavyo na pia bara zima la Afrika."
Ghana, timu pekee kutoka Afrika iliyovuka hatua ya makundi lakini ikang'olewa na Uruguay kwenye robo fainali katika mechi iliyokuwa na utata wa aina yake.
Mashabiki wa timu ya Ghana
Ni mara ya kwanza kwa Kombe la Dunia kufanyika barani Afrika, na wengi walikuwa na matumaini timu moja kutoka barani humo ingefika nusu fainali.
Ghana walitoka sare ya 1-1 na Uruguay katika muda wa kawaida, lakini sekunde za mwisho za muda wa nyongeza Asamoah Gyan alipokosa penati baada ya Luis Suarez wa Uruguay kuzuia kwa mikono mpira uliokuwa unaingia golini.
Black Stars walijikuta wakitolewa kwenye michuano hiyo baada ya Gyan kukosa penati hiyo kisha zilipopigwa penati tano tano, Ghana walipoteza mbili dhidi ya Uruguay waliokosa moja.
Kulikuwa na vilio vya furaha katika uwanja wa ndege wa Accra wakati ndege ya wachezaji wa Black Stars walipotua siku ya Jumatatu jioni.
Mashabiki wa mpira, wengi ambao waliwasili saa kadhaa kabla ya timu hiyo kufika, walipunga bendera za taifa za Ghana na kupuliza vuvuzela kuwalaki mashujaa wao.
Nahodha wa Ghana, Stephen Appiah alisema: "Tumejitahidi kwa kadri ya uwezo wetu lakini hatukuwa na bahati, hata hivyo tutakwenda Brazil mwaka 2014 na tutakuwa washindani wakuu."
Awali Rais John Evans Mills aliwasihi Waghana kutowabughudhi wachezaji licha ya kukatishwa tamaa na kushindwa kwao.
Amesema, " Ni bora tuendelee kuwaunga mkono na tuwaonyeshe kuwa tumeshukuru kwa hatua waliyofika."
" Katika mechi ya Ijumaa, kulikuwa kuwepo mshindi mmoja tu na kwa bahati mbaya, haikuwa Black Stars."
" Ndoto zatimia"
Siku ya Jumapili, watu walijikusanya kuishangilia timu ya Ghana walipokuwa wakifanya ziara mjini Johannesburg.
Awali Jumamosi, timu hiyo ilikutana na aliyekuwa mke wake Nelson Mandela, Winnie Madikizela-Mandela mjini Soweto, kabla ya kumtembelea Bw Mandela nyumbani kwake mjini Johannesburg.
"Ni bora tuendelee kuwaunga mkono na tuwaonyeshe kuwa tumeshukuru kwa hatua waliyofika" Rais wa Ghana, John Evans Mills
Baada ya kukutana kwao, ofisi ya Bw Mandela ilisema, " Waliwakilisha bara la Afrika vilivyo na licha ya kutofuzu kwa nusu fainali wanaweza kurejea nyumbani kwa kujiamini."
Golikipa Richard Kingson alisema, " Nimefurahi kukutana na mtu muhimu kama Rais Mandela. Nilikuwa naye, nikimshika mkono, Nimefurahi sana kukutana naye uso kwa uso."
Kevin-Prince Boateng alisema: " Ni ndoto iliyotimia. Ni jambo zuri sana kwetu. Tumefurahi sana kukutana na mtu huyu. Ni mtu mashuhuri."  BBC SWAHILI.

0 comments:

Post a Comment