SONYA_FLAWLESS_IMG
WE CREATE GREATNESS. | Professional Networker | Global Business Builder | Health And Wellness Coach | YOUR DREAM OUR PLAN.

Sunday, May 9, 2010

Barabara za juu Dar es Salaam sasa mwaka huu

UJENZI wa barabara mbili za juu (fly-over) ili kupunguza foleni katika Jiji la Dar es Salaam utaanza baadaye mwaka huu baada ya taasisi za fedha za kimataifa kukubali kutoa fedha kugharamia mradi huo.

Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Adam Kimbisa aliyasema hayo Dar es Salaam alipokuwa akizungumza katika kipindi cha Kumepambazuka kinachorushwa na televisheni ya ITV, jana asubuhi.

Alisema Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) wamekubali kutoa fedha za kugharamia ujenzi wa barabara hizo na tayari Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam imewasilisha bajeti ya ujenzi wa barabara hizo katika maeneo ya Ubungo na Tazara.

“Hatua hii imekuja baada ya Jumatatu iliyopita Jiji kuandaa mkutano mkubwa wa kimataifa wa kuzungumzia changamoto zinazolikabili Jiji la Dar es Salaam ambapo viongozi wa mashirika haya ya fedha walihudhuria,” alisema Kimbisa.

Alisema ingawa ujenzi utaanza mwaka huu lakini utakamilika ndani ya kipindi cha miaka miwili au miwili na nusu, hatua itakayosaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza foleni katika barabara kubwa nne za Nyerere, Morogoro, Kilwa na Bagamoyo.

“Barabara hizi nne ndizo zinazotumika kuwaleta watu mjini asubuhi na kuwarejesha nyumbani jioni. Kwa ukuaji wa Jiji la Dar es Salaam hivi sasa barabara hizi hazitoshelezi na tumeona ni lazima tuanze kuchukua hatua madhubuti za kukabiliana na tatizo hili kwa kujenga barabara za pembeni ili kusaidia,” alisema Kimbisa.

Alisema serikali imeamua kujenga barabara hizo mbili kwanza kutokana na unyeti na ulazima wa kuwa na barabara za juu katika maeneo hayo ya Ubungo na Tazara.

Alisema unyeti wa eneo la Ubungo unatokana na barabara ya Morogoro kutumika na magari yote yanayotoka mikoani na nchi jirani kuja Dar es Salaam na Tazara kunatokana na barabara ya Nyerere kutumiwa na watu wengi wakiwemo wanaosafiri kwenda au kutoka nje ya nchi kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere.

Alisema Jiji pia limeainisha baadhi ya barabara za pembeni zitakazosaidia kupunguza foleni katika barabara hizo kuu nne za Nyerere, Morogoro, Bagamoyo na Kilwa.

Katika hatua nyingine Kimbisa alisifu ukarimu uliooneshwa na wakazi wa Dar es Salaam wakati wa Mkutano wa Kiuchumi wa Dunia (WEF), uliofanyika kwa siku tatu kuanzia Mei 5 hadi Mei 7, mwaka huu.
Imeandikwa na Na Oscar Mbuza.

0 comments:

Post a Comment